Wednesday, September 26, 2012

Vita CCM

Best Blogger Tips
HALMASHAURI Kuu ya CCM (Nec), imetangaza majina ya wagombea walioteuliwa kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya chama hicho, huku ikionyesha kuwa uchaguzi huo utakuwa na mchuano mkali.

Katika orodha iliyotolewa jana, baadhi ya makada wake maarufu akiwamo Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono na Salum Londa wametupwa.

Mchuano mkali unaonekana kuwapo kwenye nafasi ya ujumbe wa Nec Mkoa wa Manyara ambako Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye anachuana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk Mary Nagu.

Mchuano huo unatarajiwa kuwa mkali katika nafasi ya uenyekiti kwenye baadhi ya mikoa kutokana na kupitishwa kwa majina ya makada wake maarufu. Mwanza ni miongoni mwa mikoa hiyo kwani Nec imepitisha jina la Waziri wa zamani wa Maliasili na Utalii, Anthony Diallo ambaye atachuana na Clement Mabina anayetetea nafasi hiyo.

Makada hao watapata ushindani mkali kutoka kwa Zebedayo Athumani, Joseph Yaredi na Mashimba Hussein Mashimba.

Dar es Salaam nako kunatarajiwa kuwa na mchuano mkali kwani mwenyekiti wa sasa, John Guninita atachuana na Mkuu wa Kitengo cha Uchaguzi Makao Makuu ya CCM, Matson Chizzi na kada mwingine, Ramadhan Madabida. Godfrey Mwalusamba, Harold Adamson na Paul Laizer wanawania nafasi hiyo mkoani Arusha.

Vita nyingine kali ipo kwenye Jumuiya ya Wanawake wa Tanzania (UWT), ambako Mwenyekiti wa sasa, Sofia Simba ambaye pia ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto anachuana na Mbunge wa Same Mashariki, Anna Kilango Malecela na Mbunge wa Viti Maalumu, Mayrose Majige.

Katika Jumuiya ya Wazazi, Mkono ambaye alikuwa akiwania nafasi hiyo ametupwa na kuwaacha Abdallah Bulembo, Martha Mlata na kada wa siku nyingi, John Barongo kuchuana.

Awali, Mkono alikatwa jina lake na Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya hiyo na kutangaza hali ya hatari akisema asipopitishwa patachimbika. Jina lake lilirejeshwa na Kamati ya Usalama na Maadili kabla ya kukatwa tena na Kamati Kuu.

Alipoulizwa jana kuhusu kuondolewa katika kinyang’anyiro hicho, Mkono alisema: “Nimekubaliana na uamuzi wa chama na nitaendelea kuwa mwanachama wa CCM. Nimelelewa na kukulia CCM na nitaendelea kubaki CCM nikiwa mwanachama mtiifu.”

Katika Jumuiya ya Vijana (UVCCM), mchuano mkali unaonekana kuwa katika nafasi ya makamu mwenyekiti kwani mmoja wa wagombea waliopitishwa, Paul Makonda anaaminika kuwa na nguvu kubwa kutoka katika kundi la wabunge na mawaziri wapambanaji wa ufisadi. Makonda anawania nafasi hiyo pamoja na Mboni Mhita na Ally Hapi.

Nafasi ya Mwenyekiti UVCCM inawaniwa na Sadifa Juma Khamis, Rashid Simai Msaraka na Lulu Mshamu Abdallah.

Waziri Mkuu aliyejiuzulu na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa atachuana na Dk Salash Toure na Nanai Kanina kwenye nafasi ya ujumbe wa Nec kupitia Wilaya ya Monduli.

Wagombea wa ‘kundi la kifo’
Vigogo kadhaa wamepitishwa kuwania nafasi 10 za Nec, wakiwamo baadhi ya mawaziri na viongozi wa juu wa chama hicho.

Miongoni mwao ni Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Shy-Rose Bhanji, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk David Mathayo David, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi, Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, January Makamba, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe na Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama.

Wengine ni Katibu wa Fedha na Uchumi CCM, Mwigulu Nchemba, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Uhusiano, Stephen Wassira, Waziri wa Habari, Michezo, Utamaduni na Vijana, Dk Fenela Mukangara na Katibu Mkuu wa UVCCM, Martin Shigela.

Kwa upande wa Zanzibar, nafasi 10 za Nec kupitia kapu zinawaniwa na Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan.

Katika orodha hiyo wamo, Waziri wa Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hussein Mwinyi, Waziri wa zamani wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano, Mohamed Seif Khatib, Waziri wa Fedha na Mipango wa Zanzibar, Omar Yussuf Mzee na Naibu Waziri wa Fedha wa zamani, Abdisalami Issa Khatib.

Familia ya Kikwete
Katika uteuzi huo wa wagombea, majina matatu ya wagombea kutoka katika familia ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete yamepitishwa.

Waliopitishwa ni pamoja na mkewe Salma Kikwete ambaye anakuwa mgombea pekee katika nafasi ya ujumbe wa Nec Lindi Mjini na Ridhiwan Kikwete ambaye pia ni mgombea pekee wa nafasi hiyo katika Wilaya ya Bagamoyo.

Mbali ya hao, Nec pia imepitisha jina la Mohamed Mrisho Kikwete kuwania nafasi ya uenyekiti wa Wilaya ya Bagamoyo.

Vigogo watemwa
Nec imewatema vigogo kadhaa, baadhi yao ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kigoma, Azim Premji na aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Vicky Nsilo-Swai ambaye alikuwa anagombea ujumbe wa Nec kupitia Wilaya ya Hai na kada wa siku nyingi, Salum Londa.

Pia wamo wabunge, Sarah Msafiri, Munde Tambwe, Deo Filikunjombe na Victor Mwambalaswa.Wengine waliotemwa ni Hussein Bashe na hasimu wake mkubwa kisiasa Dk Hamis Kigwangalla, Jamali Kassim, Anthony Mavunde na Emmanuel Nzungu, ambaye aliomba kugombea Uenyekiti Wilaya ya Ilemela, Mwanza.

Mgeja chupuchupu
Mwenyekiti wa sasa wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja aliponea chupuchupu kutemwa baada ya Nec kurejesha jina lake kwenye orodha ya wagombea lililokuwa limeondolewa na vikao vya awali.Taarifa za kuondolewa jina la Mgeja zilivuja tangu juzi wakati kikao cha Kamati Kuu kilipoketi ikidaiwa ni kutokana na malumbano kati yake na Mbunge wa Kahama, James Lembeli.

Inadaiwa wakati wa kujadiliwa Mgeja, Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete alitoka kwenye kikao na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na kumwachia kiti Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Pius Msekwa.

Baada ya mjadala mrefu wa kumtetea Mgeja kwamba hakutendewa haki, Msekwa alifikia uamuzi wa kurejesha jina.

“Baadhi ya waliomtetea ninaokumbuka ni Dk Makongoro Mahanga na Peter Serukamba, lakini wakati wa mjadala wa Mgeja, Mwenyekiti (Kikwete) na Nape walikwenda chemba, kiti akaachiwa Msekwa,” kilisema chanzo chetu.

Awali, kada mkongwe wa chama hicho, Kingunge Ngombale - Mwiru aliituhumu Kamati Kuu kwamba imevunja kanuni za uchaguzi kwa kuteua majina zaidi ya matatu kwenye nafasi moja.

Hata hivyo, inadaiwa Msekwa alimsomea kanuni moja baada ya nyingine zinazohusu uteuzi hali iliyoonyesha kama kumweka darasani na hatimaye ikabainika hakuna kanuni iliyovunjwa.Hoja hiyo ilitokana na baadhi ya mikoa kwenye nafasi moja kusimamisha wagombea zaidi ya watatu kama nafasi ya mwenyekiti mkoa wa Mwanza.

Hatua hiyo inadaiwa inalenga kuondoa matokeo ya kupanga kwa baadhi ya wagombea na kwamba, kwa hali hiyo mshindi hawezi kupatikana kwa mzunguko wa kwanza.

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu Mstaafu wa CCM, Yusuf Makamba anadaiwa kushambulia mtandao uliokuwa umejipanga na kuweka wagombea wao hata kama hawana sifa.“Yule mzee (Makamba) amewachana-chana vibaya, anasema hapa tunasajili timu, kama majina hayafai yaondolewe,” kilidokeza chanzo na kuongeza kwamba hoja hiyo iliungwa mkono na kada mkongwe wa chama hicho, Mzee Peter Kisumo.
Chanzo: Mwananchi

Kikwete: Anayetaka kuondoka CCM ‘ruksa’

Best Blogger Tips
 MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete amewatolea uvivu wagombea wa nafasi mbalimbali ambao majina yao yamekatwa, akisema wanaotaka kukihama chama hicho kwa sababu wametoswa, waondoke haraka.

Licha ya kuwatakia safari njema, Rais Kikwete aliwatupia lawama baadhi ya wanaCCM ambao wameripotiwa kuendesha malumbano na kugeuza uchaguzi huo kama uwanja wa vita.

Akifungua kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM (Nec) jana, Rais Kikwete alisema kumekuwapo na taarifa mbalimbali ambazo zimemfikia pia kwamba baadhi ya wanachama wanatishia kukihama chama hicho kama majina yao yatakatwa.

“Wako wenye ndimi mbili ambao wanasema kuwa wasipoteuliwa wanaweza kuondoka. Ah! Mimi nasema watangulie huko maana inaonyesha kuwa walishaandaa maeneo ya kwenda,” alisema Rais Kikwete huku akishangiliwa na wajumbe wa Nec.

Alisema CCM kinayo taarifa kuhusu watu kugombana na hata kutoleana silaha, jambo alilosema linashangaza, huku akihoji kuna nini katika uongozi tena Nec?

“Uchaguzi usigeuzwe uwanja wa fujo. Wengine wanatoleana silaha kama majembe, ngumi na silaha nyingine, hivi wanagombana nini huko? Uchaguzi usigeuzwe kuwa ni uwanja wa vita.” alisema.

Hivi karibuni, baadhi ya makada wa chama hicho wamekuwa wakitoa kauli mbalimbali za kukitishia chama hicho akiwemo Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono ambaye alikaririwa akisema kama jina lake halitapitishwa, patachimbika.

Mbunge huyo alisema hayo siku chache baada ya jina lake kutupwa na Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi iliyokuwa ikipitia na kuteua wagombea watatu kwa ajili ya kuwania nafasi ya mwenyekiti wa jumuiya hiyo.

"Hapatatosha CCM," alisema Mkono alipoulizwa na waandishi wa habari kuhusu kutoswa kwake katika mchujo wa awamu hiyo ya awali.

Ingawa Rais Kikwete hakutaja majina, Mbunge wa Nzega Dk Khamis Kigwangallah na Hussein Bashe nao waliripotiwa kutoleana maneno makali hata kuonyeshana bastola, huku Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja na Mbunge wa Kahama, James Lembeli wakiendesha malumbano kwa muda mrefu.

Inadaiwa kuwa majina hayo yote na ya vigogo wengine yamekatwa na jana baadhi yao walikuwa wanadai kuwa CCM kinataka kuzalisha upinzani ambao utakisababishia kushindwa katika safari yake kisiasa hasa katika mfumo huu wa vyama vingi.

Licha ya makaripio hayo, Rais Kikwete alibainisha kuwa CCM kinasemwa na watu kuwa kinakithiri rushwa katika chaguzi zake hivyo akawataka wagombea kubadilika kabla ya kukamatwa na Takukuru.

“Zipo taarifa ingawa hatujazithibitisha kwamba wapo baadhi ya wagombea wanamwaga fedha sijawahi kuona…

Takukuru wapo wanaendelea na kazi. Chama chetu kinasemwa tujipe fursa ya kubadilika, tusisubiri kukamatwa na kuanza kuilaumu PCCB.”

Kuhusu uteuzi wa wagombea wa nafasi mbalimbali, Rais Kikwete alisema katika uchaguzi huo, wamejitokeza watu wengi tena vijana wasomi na kwamba Kamati ya Usalama na Maadili na Kamati Kuu, zimewapandisha na kuwakata waliotumikia chama muda mrefu.

“Kama hukuteuliwa kuna mawili, ama nafasi zimejaa au hufai una upungufu kidogo na huo ni utaratibu wa chama siyo kuoneana,” alisema Rais Kikwete huku akishangiliwa.

Alisema katika uteuzi huo vijana watapewa nafasi zaidi kutokana na ukweli kuwa, chama bila ya vijana hakiwezi kuwa imara kwa sababu ndiyo nguvu ya ushindi.

“Hao watakaoachwa watambue kuwa tunafanya hivyo kwa ajili ya kutengeneza timu ya ushindi ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2014 na Uchaguzi Mkuu wa 2015 kwa Bara na Visiwani, hivyo kuachwa jina lako isiwe nongwa,” alisema na kuongeza:

“Lazima tukipe chama chetu watu wa kushinda… Lazima tutambue sasa tunaunda timu ya ushindi wa chama siyo ushindi wa mtu.”

Hata hivyo, Rais Kikwete alitoa angalizo kuwa anajua kikao cha Halmashauri Kuu kingekuwa na mjadala mzito, lakini lazima wakipe chama watu wa kushinda.

Majina manne
Kamati Kuu ya CCM, inadaiwa kupendekeza majina ya wagombea wanne kwenye jumuiya zake, tofauti na kanuni ya chama hicho ya nafasi moja kuwaniwa na watu watatu.

Kikao chake kilichomalizika juzi usiku, kinadaiwa kubadili kanuni ya kupendekeza wagombea watatu kwa nafasi moja na kwamba, hivi sasa mapendekezo hasa kwenye jumuiya ni wagombea wanne.

Taarifa kutoka ndani ya kikao hicho zilidai kuwa, hatua hiyo inalenga kutoa ushindani kwa wagombea.

Hata hivyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipotakiwa kuzungumzia suala hilo hakukanusha wala kukubali zaidi ya kusema kwamba hata kama utaratibu huo umetumika siyo mara ya kwanza kwa chama hicho.

Alisema kama Jumuiya ya Vijana wanaojitokeza lengo lao linakuwa kupata uzoefu na kwamba, idadi ya majina inategemeana na busara za kikao kinavyoona ili kutoa nafasi kwa wagombea kujipima.
Chanzo: Mwananchi

Tuesday, September 18, 2012

Madaktari waliogoma waiangukia serikali

Best Blogger Tips
MADAKTARI waliokuwa kwenye mafunzo kwa vitendo ambao Serikali iliwafutia vibali vya kazi, wamesalimu amri na kuamua kumuangukia aliyekuwa mwajiri wao ili awarudishe kazini.

Serikali iliwafukuza kazi madaktari hao baada ya kutangaza mgomo usio na kikomo Juni mwaka huu, hadi madai yao yatakapofanyiwa kazi ambapo mgomo huo ulisababisha vifo kwa baadhi ya wagonjwa waliokosa huduma za matibabu.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari walioathirika na mgomo, Bw. Paul Swakala, alisema wameamua kuomba msamaha kwa Rais Jakaya Kikwete na Watanzania wote baada ya kubaini kuwa, wagonjwa wengi waliathirika na mgomo huo.

Alisema walishindwa kuuepuka mgomo huo kutokana na mazingira ya wao kufanya kazi na Madaktari Bingwa kwani mikataba yao, haikuwaruhusu kufanya kazi ya kutoa matibabu peke yao.

“Tunafahamu kuwa, Watanzania wengi waliathirika mgomo ule, tunawaomba radhi sana kwa usumbufu walioupata na tunakiri kuwa kila mmoja wao alichokizwa na uamuzi wetu.

“Japo nchini kwetu utamaduni wa kuomba radhi hadharani haupo, sisi tumeamua kufanya hivi kwa sababu tumekosa na hakuna binadamu aliye kamili wote tunakasoro,” alisema Bw. Swakala.

Aliongeza kuwa, wanatambua na kuunga mkono juhudi za Rais Kikwete katika kuboresha huduma za afya nchini licha ta changamoto nyingi zinazoikabili sekta hiyo.

“Tunamuomba radhi sana Rais Kikwete na Serikali yake kwa usumbufu uliosababishwa na mgomo, pia tunatambua jitihada zake za kutafuta suluhu ya mgomo uliopo,” alisema.

Aliwahakikishia Watanzania kuwa, kuanzia sasa hawako tayari kushiriki mgomo kwa namna yoyote kwabni kufanya hivyo ni kuweka rehani maisha ya wagonjwa.

Bw. Swakala alisema wanajutia kosa hilo na wako tayari kulejea kazini ili kuwahudumia Watanzania kwa moyo mweupe na wanayo dhamira ya kounana na Rais Kikwete ana kwa ana ili kumuomba radhi.

Akijibu maswali ya waandishi wa habari, Bw. Swakala alisema madaktari ambao wamesaini fomu za kuomba radhi ni 200 kati ya 364 waliofutiwa vibali vya kazi.

“Mimi nimesoma kwa gharama za sh. milioni 35, sioni faida ya kukaa mtaani wakati Watanzania wakiendelea kupata  shida ya matibabu,” alisema Bw. Swakala.

Akizungumzia suala la vifaa ambalo ni moja ya sababu iliyowafanya wagome, Bw. Swakala, wao wanaamini Rais Kikwete na Serikali yake itaboresha mazingira ya huduma za afya.

“Chama cha Madaktari nchini (MAT) ni cha hiari, hatuungani na msimamo wao, wanachama walionao ni madaktari wenye usajili wa kudumu si kama sisi, hatulazimishwi kujiunga nao,” alisema.

Madaktari hao walifanya mgomo huo ili kuishawishi Serikali iboreshe mazingira ya kazi, nyongeza ya mishahara na marupurupu mengine.
Source: Tanzania Daima

Sunday, September 16, 2012

UWT kwawaka moto

Best Blogger Tips
MAPENDEKEZO ya Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Umoja wa Wanawake (UWT) wa CCM ya majina ya wagombea nafasi ya uenyekiti wa jumuiya hiyo ngazi ya taifa, yameibua mlolongo wa tuhuma kuwa yalifikiwa kwa upendeleo, rushwa na woga.

Tuhuma hizo zimetolewa na baadhi ya walioomba kuteuliwa kuwania nafasi hiyo, ambao majina yao hayakupendekezwa na kamati wanayodai kuwa ilifanya kazi kwa woga na kuwapendelea baadhi ya wagombea baada ya kushawishiwa kwa rushwa.

Mbali ya malalamiko ya wagombea, taarifa kutoka ndani ya UWT zinaeleza kuwa, uteuzi wa majina yaliyopendekezwa na kamati ya utekelezaji na kupelekwa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM umeibua ufa baina ya wanajumuiya hiyo kwa kile kinachoelezwa baadhi yao kujiona wanatengwa kwa sababu hawana watu wa kuwapigania dhidi ya wake wa vigogo wanaodaiwa kuogopwa na kutetewa na waume zao.

Mmoja wa wagombea ambaye jina lake halikupendekezwa, Hamida Thabit, katika mahojiano yake na gazeti hili kuhusu mwenendo wa mchakato wa uteuzi alisema ulikuwa wa hovyo kwa sababu haukuzingatia sifa na uwezo wa waombaji.

Alisema waombaji wenye sifa majina yao hayakupendekezwa kwa sababu hawakuwa na pesa za kuwafurahisha wajumbe, na majina ya waombaji ambao waume zao wana sauti ndani ya chama yalipitishwa kwa woga.

“Sijaridhika na mapendekezo ya kamati. Siyo kwamba nina uchu wa madaraka, lakini wakati mwingine ukiona mambo yanakwenda kombo kiasi cha kutisha ni lazima kusema. Na ninasema ili NEC ilione hili, itende haki kwa sababu UWT ni waoga.

“Baadhi yetu majina yetu hayakupendekezwa kwa sababu hatuna pesa, hatuna watu wa kututetea, hatuna wanaume wenye nyadhifa au sauti ndani ya chama. Ni aibu kwa jumuiya iliyokomaa kama UWT kuchagua watu kwa kuwaogopa, eti wasipochaguliwa watapiga kelele.

“Wabunge wenye majimbo, wana kazi za kila siku za kusimamia majimbo yao, bado wanataka na kazi ngumu ya kuongoza umoja huu na majina yao yanapitishwa, hiyo maana yake nini? Wanaachwa watu wenye sifa, wanaoijua UWT,” alisema Hamida.

Alisema mwenendo wa sasa wa CCM unaonekana kuwa wa kifamilia zaidi kwa sababu licha ya kuwa na wanachama wengi wenye sifa na uwezo wa kushika nafasi za uongozi, bado nafasi hizo zinatolewa kwa kujuana na hasa kwa kuangalia wake wa vigogo.

Alitolea mfano wa Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango, kuwa ni mbunge wa jimbo ambaye ana jukumu la kuwatumikia wapiga kura wake, hivyo hapaswi kukabidhiwa jukumu lingine la kuongoza UWT kwa sababu majukumu yote ni mazito.

Pia alisema Maryrose Majinge hakupaswa kupendekezwa kwa sababu hana sifa zinazostahili kuwa kiongozi wa juu wa umoja huo.

“Anne Kilango ni mbunge wa jimbo, anawajibika kwa karibu sana kwa wananchi wa jimbo lake, lakini bado anataka uenyekiti wa jumuiya. Majukumu yote ni mazito, kwanini yeye tu majukumu hayo?

“Sophia Simba ni sawa kwa sababu yeye ni mwenyekiti hivyo anatetea kiti chake na anao uzoefu wa uongozi ndani ya jumuiya, lakini hata huyu Maryrose, ametokea umoja wa vijana moja kwa moja amerushwa hadi kwenye uenyekiti, aanzie chini ajifunze na kupata uzoefu.

“Huu ni upendeleo wa wazi kabisa, unajua ukiwa na watoto watatu halafu ukawa unampendelea mmoja tu, wengine lazima watalalamika na itafika mahali watapachukia nyumbani, huko ndiko tunakokwenda.

“Kwa sababu lazima ieleweke kuwa kujua kupiga kelele siyo ujuzi wa kiutendaji, kupiga kelele bungeni siyo kigezo cha kuwa kiongozi bora,” alisema.

Alipoulizwa kama ana mpango wa kukata rufaa kupinga mapendekezo hayo, alisema hana mpango huo kwa sababu anaamini hakuna kitakachofanyika isipokuwa anabaki na matumaini NEC itatenda haki.

Mgombea mwingine aliyelalamikia mapendekezo ya kamati ya utekelezaji ya UWT ni Hilder Kitana, ambaye alisema ingawa anayaheshimu maamuzi ya kamati hiyo, amesikitishwa na kitendo chake cha woga.

Kitana alisema kamati hiyo imewaacha baadhi ya waombaji wenye sifa na kuchukua majina ya watu ambao hawana rekodi ya uongozi ndani ya jumuiya, lakini pia wenye majukumu ya kila siku kwa nafasi ambazo tayari wanazo.

“Wameamua wamependekeza majina hayo sawa, nayaheshimu. Lakini nimesikitishwa na woga wa kamati hii. Tukienda kwa kuogopana kama walivyokuwa wanasema ndani ya kamati hiyo hatutafika, tunaiua jumuiya.

“Mimi nimekuwa Mjumbe Kamati Kuu ya UWT, nimekuwa Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Dar es Salaam, ninaijua jumuiya, sina jukumu kwa sasa linalonibana moja kwa moja zaidi ya biashara zangu, halafu jina langu linakatwa kwa sababu wanasema wakimuacha Kilango, anaongea sana na mke wa mtu mkubwa itakuwa matatizo, atapiga kelele hadi kwenye vyombo vya habari, huu ni udhaifu mkubwa,” alisema Kitana.

Kwa upande wake, Maryrose Majinge, alisema licha ya jina lake kupendekezwa, anasubiri maamuzi ya NEC.
Alisema nafasi za uongozi ndani ya CCM zinapaswa kuzingatia uwezo wa utendaji badala ya kuchagua watu kwa sifa ya kuzungumza au kwa majina ya wenzi wao.

Wiki iliyopita, kamati ya utekelezaji ya UWT iliyoketi mjini Dodoma ilipendekeza majina ya wanachama wake watatu kwenda NEC ya CCM kwa ajili ya kuwania uenyekiti wa jumuiya hiyo. Waliopendekezwa ni Mwenyekiti wa sasa, Sophia Simba, Anne Kilango na Maryrose Majinge.
Chanzo: Tanzania Daima

Wednesday, September 12, 2012

Balozi wa Marekani auawa Libya

Best Blogger Tips
 Balozi wa Marekani nchini Libya ameuawa baada ya kushambuliwa na watu waliokuwa wamejihami na kuvamia ubalozi wa Marekani Mashariki mwa mji wa Benghazi.

Balozi J Christopher Stevens, ni miongoni mwa maafisa wengine wa ubalozi waliouawa kufuatia maandamano kuhusu filamu iliyotolewa nchini humo ikimkejeli Mtume Muhammad.

Idara ya mambo ya ndani nchini Marekani, imethibitisha tu kifo cha afisaa mmoja wa ubalozi huo ingawa bado haijataja jina lake.

Maandamano ya kupinga filamu hiyo pia yalifanyika mjini Cairo dhidi ya ubalozi wa Marekani.
Wakati huohuo, waziri wa mambo ya nje wa Marekani Bi. Hilary Clinton, amelaani mashambulizi hayo.

Serikali ya Libya imetaja shambulio hilo kama kitendo cha uoga.
Ubalozi huo uliteketezwa na watu waliojihami kwa bunduki kulalamikia filamu moja iliyotengenezewa nchini Marekani ambayo wanasema inamdhihaki Mtume Mohammed.

Wanamgambo hao wanaoripotiwa kuwa na ufungamano na kundi la waislamu wenye msimamo mkali walitumia maguruneti ya kurushwa kwa roketi kuvamia ubalozi huo kabla ya kuiteketeza. Maafisa wa Libya wameiambia BBC kwamba hali imetulia kwa sasa.

Machafuko hayo ya Libya yalijiri saa kadhaa baada ya maelfu ya waandamanaji kukusanyika nje ya ubalozi wa Marekani mjini Cairo kuelezea hasira zao kuhusu filamu hiyo kumhusu Mtume Mohammed.

Kwa wakati mmoja waandamanaji hao waliingia ndani ya ubalozi huo na kuichana bendera ya Marekani na kurejesha yao.
Chanzo: BBC

Wednesday, September 5, 2012

Al-Senussi akabidhiwa kwa watawala wa Libya

Best Blogger Tips
 Serikali ya Mauritania imewakabidhi maafisa wa utawala wa Libya aliyekuwa mkuu wa ujasusi nchini humo, Abdullah al-Senussi.

Libya inataka kumfungulia mashtaka bwana Senussi kwa makosa aliyoyafanya chini ya utawala wa hayati Muamar Gaddafi.

Mapema mwezi huu rais wa Mauritania, Mohamed Ould Abdel Aziz alisema kuwa bwana Sanusi aliyekuwa amekimbilia nchini humo, sharti kwanza akabiliwe na sheria kwa makosa ya kuingia Mauritania kinyume na sheria.

Senussi alitoroka Libya baada ya mapinduzi ya mwaka jana ambayo yalimng'oa mamlakani Muammar Gaddafi.

Pia anatakiwa na Ufaransa pamoja na mahakama ya kimataifa kuhusu haki za bianadamu ICC kwa makosa ya kukiuka haki za binadamu.

Ripoti za kukabidhiwa kwake kwa watawala wa Libya, zilitolewa na televisheni ya taifa pamoja na shirika rasmi la habari la Mauritania.

Kulingana na ripoti, bwana Senussi alikabidhiwa kwa wajumbe wa Libya walioongozwa na waziri wa sheria na haki wa nchi hiyo. Lakini hadi sasa bwana Senussi hajulikani aliko.
Chanzo: BBC

Monday, September 3, 2012

Mauaji Iringa yamtesa IGP

Best Blogger Tips
 TUKIO la kuuawa kwa mwandishi wa habari wakati polisi wakipambana na wafuasi wa Chadema mkoani Iringa, limelitikisa jeshi hilo na jana Mkuu wake (IGP), Said Mwema alilazimika kujifungia na vigogo wa polisi Mkoa wa Iringa kujadili suala hilo.

Wakati IGP Mwema akifanya mkutano huo, uliodumu kwa zaidi ya saa mbili na nusu, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi amelazimika kukatisha ziara yake ya kikazi Afrika Kusini na kurejea nchini kushughulikia suala hilo.

Mwema alienda Iringa jana na kuitisha mkutano huo uliowahusisha pia viongozi wa Chadema, akiwamo Katibu Mkuu wake, Dk Willibrod Slaa katika mazingira yaliyoelezwa kuwa na ulinzi mkali.
Hii ni mara ya kwanza IGP Mwema kwenda mwenyewe kwenye mikoa kunakotokea vurugu kati na vyama vya siasa na baadaye mauaji ya raia.

Julai 15, mwaka huu vurugu za aina hiyo zilitokea mkoani Singida ambako Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM Kata ya Ndago wilayani Iramba, Yohana Mpinga aliuawa kwa kupigwa na silaha za jadi.

Pia mkoani Morogoro, Ally Zona aliuawa katika vurugu zilizoibuka baina ya polisi na wafuasi wa Chadema katika haraka za jeshi hilo kuwasambaratisha wafuasi hao kwa kile ilichoeleza kuwa maandamano yao yalipigwa marufuku.
Katika vurugu zote hizo, IGP amekuwa akituma wawakilishi au kutumia polisi kwenye mkoa husika kushughulikia matatizo hayo.

Makubaliano ya kikao
Taarifa kutoka ndani ya kikao hicho zimeeleza kuwa polisi imekubaliana na Chadema na Umoja wa Vyama vya Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) kusitisha majadiliano yote yanayohusu kifo cha mwandishi huyo hadi mazishi yake yatakapokamilika.

Mwenyekiti wa UTPC, Kenneth Simbaya alisema baada ya mkutano huo kuwa wamekubaliana kuwa na mkutano mwingine baada ya shughuli za mazishi kukamilika.

“Tulichoomba kifanyike ni kwamba, tumzike mwenzetu halafu majadiliano mengine juu ya ilikuwaje kwa nini na nini kifanyike kwa siku za usoni yatakuja,” alisema Simbaya.
Alisema sasa wanasubiri mwili wa Mwangosi ufanyiwe uchunguzi na wataalamu kutoka Dar es Salaam kabla ya kukabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya maandalizi ya mazishi.

Katibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Iringa (IPC), Francis Godwin alisema uchunguzi wa awali wa IPC unapingana kwa asilimia zote na taarifa ya jeshi hilo kwa kuzingatia taarifa zilizotolewa na baadhi ya waandishi waliokuwapo katika tukio hilo.

“Taarifa kutoka katika vyanzo vyetu zinaonyesha kwamba Mwangosi alipigwa kwa virungu kabla ya kulipuliwa na bomu hilo ambalo kwa vyovyote vile mhusika wake mkuu anaweza kuwa jeshi hilo na ili taarifa hiyo potofu isiendelee kuugubika umma, IPC imeamua kutoa tamko linalolenga kuviarifu vyombo huru viingilie kati uchunguzi,” alisema Godwin.

Nchimbi akatisha ziara
Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi jana alilazimika kukatisha ziara yake ya kikazi, Afrika Kusini na kurudi nchini ambako pamoja na mambo mengine, atazungumza na waandishi wa habari leo kuhusu tukio hilo.

Nchimbi anarejea nchini wakati Naibu wake, Pereira Ame Silima akikataa kulizungumzia akisema uchunguzi umeshaanza.

Silima alisema tukio hilo linachunguzwa kwa pamoja kati ya Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba na IGP Mwema... “Mwema na Manumba wanaelekea Iringa ikiwa ni sehemu ya uchunguzi wa tukio hilo na baadaye ndipo jeshi la polisi litaweza kueleza ni kitu gani hasa kimetokea.”

Alisema kwa sasa lolote litakalozungumzwa juu ya tukio hilo litakuwa ni hisia tu na ukweli utajulikana baada ya uchunguzi huo kukamilika.

Channel Ten yanena
Uongozi wa kampuni ya Africa Media Group ambao wanamiliki Kituo cha Televisheni cha Channel Ten, umeitaka Serikali kuanzisha uchunguzi huru ili kubaini sababu na mazingira ya kuuawa kwa mwandishi huyo ambaye alijiunga na kampuni hiyo mwaka 2006.

Taarifa iliyotolewa na kampuni na kusainiwa na Mhariri Mkuu wa Channel Ten, Dina Chahali imetaka uchunguzi huru kufanyika na kuhakikisha wahusika wa tukio hilo wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

“Tunalaani vikali tukio hili ambalo halikubaliki kwa jinsi yoyote ile, tunataka kuanzishwa uchunguzi huru na hatimaye nguvu za kisheria zitumike,” imesema sehemu ya taarifa hiyo.
Chanzo: Mwananchi

Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits