Monday, August 29, 2011

Familia ya Gaddafi yatorokea Algeria

Best Blogger Tips
Mke wa Kanali Gaddafi wanawe wa kiume na binti yake
Mke na watoto watatu wa kiongozi wa Libya aliye mafichoni Muammar Gaddafi wako nchini Algeria, maafisa wa Algerian wamesema.

Taarifa ya wizara ya mambo ya nje imesema mke wa kanali Gaddafi, Safia, binti yake Ayesha na watoto wa kiume Muhammad na Hannibal waliondoka Libya mapema Jumatatu.

Balozi wa Algeria katika Umoja wa Mataifa amesema walipokelewa kwa misingi ya kibinadamu.

Waasi wa Libya wamesema kuwapa hifadhi familia ya Gaddafi ni kitendo cha uchokozi, na wametaka warejeshwe nchini Libya.

Haijulikani mahali alipo Kanali Gaddafi.

Wakati huo huo waasi wamesema mtoto mwingine wa kiume wa Kanali Gaddafi, Khamis, huenda aliuawa katika mapigano karibu na Bani Walid.

Taarifa hizo zimetolewa wakati waasi wa Libya wakijaribu kumaliza upinzani uliopo katika baadhi ya maeneo ya nchi hiyo yanayomtii Gaddafi, na kujiandaa kuendelea kwenda katika mji aliozaliwa kanali Gaddafi wa Sirte ili kumalizia upinzani unaonekana kuwa ngome yake ya mwisho.

Kuwasili kwa mke wa kanali Gaddafi na watoto watatu nchini Algeria kuliripotiwa Umoja wa Mataifa na kwa viongozi wa waasi wa Libya, wizara ya mambo ya nje ya algeria imesema katika taarifa iliyotangazwa na shirika la habari la Algeria, APS.

Taarifa hiyo imesema familia ya Gaddafi walivuka mpaka kati ya Libya na Algeria Jumatatu, saa Mbili na dakika arobaini na tano za huko.

Algeria ni mahali dhahiri pa kukimbilia familia ya Gaddafi kutokana na nchi mbili hizo kuwa na mpaka mrefu na serikali ya Algeria bado halijalitambua Baraza la Mpito la Taifa la Libya.
Source: BBC

Sunday, August 28, 2011

Wananchi wamepoteza imani na CCM-Msekwa

Best Blogger Tips
Via Majira

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bw. Pius Mseka, amekiri wananchi kupoteza imani na chama hicho, kutokana na
matukio mbalimbali yanayojitokeza, huku viongozi wa chama na serikali wakishindwa kuchukuliwa hatua.

Pia alisema kutokana na hali hiyo, ndio maana katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2010, CCM ilipata ushindi wa asilimia 61 ikilinganishwa na asilimia 82 ambazo chama hicho kilipata mwaka 1995.

Bw. Msekwa, alitoa kauli hiyo jana wakati akuhojiwa na kituo cha televisheni cha Star Tv katika kipindi cha Medani za Siasa na Uchumi.

Alisema chama tawala kinapaswa kutambua kuwa kina wajibu wa kutimiza majikumu yake sasa, kwani inapofika mahala chama kikasahau wajibu wake wananchi wana haki ya kutokukichagua.

"Ili chama kichaguliwe ni lazima kioneshe kwa vitendo nia  na malengo ya kutimiza wajibu kwa wananchi, ili waweze kukiamni," alisema.

Bw. Msekwa alisema kiongozi yoyote anayeficha  ukweli kwamba wananchi wamepoteza imani na CCM, mtu huyo hayuko makini na hatakiwi kuendelea kuwa mwanachama.

Alisema kuwa kutokana na mambo yanavyoendelea  na viongozi wa serikali kushindwa kuchukua hatua ni chanzo cha wananchi kupoteza imani na chama.

Aliongeza kwa kutambua hilo, ndio maana chama kimekuja na dhana ya kujifua gamba kwa kuwataka wanaotuhumiwa kukipotezea mwelekeo chama hicho, wajiondoe wenyewe.

Hata hivyo alijigamba kwamba vyama vya upinzani kama Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) kilipata wabunge wengi bungeni kutokana na wanachama wa CCM waliokuwa wanagombea ubunge kuachwa katika kura za maoni na kukimbili upinzani.

"Ni kweli kabisa kuna baadhi ya makosa tulifanya kwa kuwapitisha wagombea wasiokubalika kwa wananchi na wale waliokubalika tuliwaacha na wao kuhamia CHADEMA na ndio hao wameshinda," alisema Bw.Pius.

Alisema vya upinzani havikuwa na uwezo wa kuwashawaishi wananchi ili wavichague, bali ilitokana na nguvu ya CCM kwa kuwa wananchi walikuwa na imani na CCM na ndio maana walichaguliwa kupitia mgongo wa CCM.

Aliongeza kuwa  CCM iliwaacha watu hao waliokimbilia  vyama vya upinzani kwa kuwa CCM ilikwishawabaini kwamba si watu wema ndani ya chama.

Bw. Msekwa alisema si  jambo jema kwa wananchi kuelekeza matatizo yote yanayotokea hivi sasa kwa chama cha mapinduzi japo kinashika dola.

Alisema kiwango cha uadilifu kwa  watendaji kwa sasa kimepungua tofauti na zamani, kwa kuwa zamani kulikuwa na chama kimoja na watendaji pia walikuwa waaminifu sana tofauti na sasa.

"Zamani uadilifu ulikuwa mkubwa kwa watendaji kwa kuwa kulikuwa na mfumo wa chama kimoja na wanachama wote macho yao yalikuwa yakilinda uadilifu tofauti na sasa", alisema.

Alisema watu wanaotakiwa kujivua gamba wapo kwenye ngazi zote.

Akizungumzia suala la makundi ndani ya chama, alisema hali hiyo inatokea wakati wa kura za maoni, ambapo majungu yanaanzia hapo na siri nyingi kuvuja na hatimaye wale walioachwa kuanzisha makundi na kuwashawishi wanachama kutowapigia kura waliopitishwa.

Alisema wanapaswa kukaa chini na kutafuta njia za kuondoa makundi ndani ya chama. "Changamoto si  kuyafumbia macho kwa kuwa yasipofanyiwa kazi yatapeleka chama pabaya," alisema.
Endelea kusoma habari hii...................
 




Friday, August 26, 2011

Maiti zagundulika hospitalini Libya

Best Blogger Tips
Zaidi ya miili ya watu 200 imepatikana katika hospitali iliyotelekezwa katika mji mkuu wa Libya Tripoli .

Mwandishi wa BBC ambaye alikwennda katika hospitali ya Abu Salim aliikuta miili ya wanaume,
wanawake na watoto kwenye vitanda na veranda na pia damu nyingi iliyotapakaa kwenye sakafu.

Madaktari na wauguzi walikuwa wameitoroka hospitali hiyo kufuatia mapigano.

Walionusurika wanasema wengi waliokuwa na majeraha waliachwa bila matibabu hadi kufa, huku wengine ikioza kando yao.

Katika mji mkuu wa Tripoli kuna taarifa kuhusu kupatikana kwa mamia ya miili ya watu waliouawa baadhi yao wakiwa wamekatwa mikono.

Pande mbili zinazohusika na mzozo nchini Libya zimekuwa zikilaumiwa kwa mauji hayo.
Chanzo: BBC

Thursday, August 25, 2011

Rais Kikwete amsimamisha Jairo

Best Blogger Tips
RAIS Jakaya Kikwete amemsimamisha kazi Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo, ili Tume atakayoiunda Spika wa Bunge, Anne Makinda imchunguze.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ameliarifu Bunge kuwa, Rais ameamuru Jairo aende likizo, na kwamba, Serikali itatoa ushirikiano wa kutosha kwa tume itakayoundwa.

Pinda ametoa taarifa hiyo kwa wabunge mjini Dodoma wakati anajibu maswali ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.

Mbowe alihoji kwa nini Jairo aendelee na kazi wakati Bunge limeamua kuunda tume kuchunguza kwa nini limedhalilishwa na pia kuchunguza mchakato wa kukusanya fedha kwa ajili ya kupitisha bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka huu wa fedha.

Mbunge huyo alimuuliza Waziri Mkuu, uhalali wa kauli ya Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo kwamba, suala la idara kuchangia fedha za kupitisha bajeti za Wizara ni la kawaida.

Kwa mujibu wa Mbowe, bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ilijadiliwa kwa siku tano, zilitumika shilingi milioni 174/- kwa ajili hiyo, lakini bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini imegharimu shilingi milioni 578/-.

Mbunge huyo wa Hai (Chadema) alimuuliza Pinda, waliohusika katika ubadhirifu wa fedha Wizara ya Nishati na Madini wamechukuliwa hatua gani za kinidhamu, na je kweli ni sera ya Serikali kuchangisha fedha kwa ajili ya bajeti za Wizara kama alivyosema Luhanjo?

Luhanjo juzi alimuamuru Jairo arudi kazini jana kwa kuwa uchunguzi uliofanywa na Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) haukumtia hatiani. Bunge jana lilisema, uamuzi alioutangaza Luhanjo umelidhalilisha na amemfedhehesha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Jairo jana alikwenda ofisini kwake wizarani jijini Dar es Salaam, wafanyakazi wakampokea kwa shangwe na vigelegele huku wakiimba kwamba wana imani naye.

Wabunge walisema jana bungeni kuwa, taarifa ya uchunguzi ya CAG kuhusu tuhuma kwamba, Jairo alichangisha Sh. Bilioni moja ili kuwezesha bajeti ipitishwe bungeni ilistahili kupelekwa bungeni waijadili kabla Serikali kutoa uamuzi.

Wabunge jana walijadili kauli ya Luhanjo kama jambo la dharura baada ya wabunge kukubali hoja ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto aliyoitoa jana asubuhi kabla ya kipindi maswali na majibu na kuifafanua baada ya Kamati ya Bunge ya Uongozi kukutana katika ukumbi wa Spika.

Zaidi ya robo tatu ya wabunge waliokuwa ukumbini wakiwemo kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) waliunga mkono hoja ya Zitto. Ndugai, alisema , hoja ya Zitto ni ya msingi kwa kuwa Bunge limedharauliwa.

“Kwa sababu Bunge ni mhimili, hatuwezi kudharauliwa kirahisi”alisema Ndugai na kusisitiza kwamba,Wabunge hawawezi kukaa kimya wakati Waziri Mkuu anadhalilishwa.

“Kama dharau inaweza ikatokea basi huko huko lakini sio ndani ya Bunge hili” amesema Ndugai baada ya wabunge kuijadili hoja ya Zitto na kusisitiza kwamba, kwa kuwa suala hilo lilianzia bungeni, taarifa ya CAG ingepelekwa kwanza kwenye mamlaka hiyo kabla ya uamuzi wa Serikali.

Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Zainab Vullu, alisema, wabunge wamepewa jukumu la kuisimamia na kuishauri Serikali kwa niaba ya wananchi hivyo kauli ya Luhanjo imewadhalilisha, na limepokwa mamlaka yake.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka, alisema, suala hilo lina maslahi kwa Taifa, taarifa ya CAG ingepelekwa kwanza bungeni itendewe haki. Sendeka alisema, Waziri Mkuu amefedheheshwa kwa kuwa kiongozi huyo wa Serikali Bungeni alisema, kama angekuwa yeye angemchukilia hatua Jairo, na pia Bunge limedhalilishwa.

Kwa mujibu wa Sendeka, kauli ya Luhanjo imelilidhalilisha Bunge na imekiuka Sheria ya Kinga na Madaraka ya Bunge na ibara ya 100 ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Mbunge huyo alitumia Kanuni 117 ya Bunge kuomba iundwe kamati teule ya Bunge kuchunguza jambo hilo ukiwemo utaratibu wa Jairo kukusanya fedha za kupitishia bajeti hasa ikizingatiwa kuwa, kila Waziri huwa na fungu la kugharamia bajeti kila idara zikiwemo fedha za kununulia mafuta.

Sendeka aliomba wabunge waunge mkono hoja yake ili kulinda hadhi ya Bunge. Wabunge walikubali isipokuwa mawaziri na manaibu mawaziri.

Wakati anatoa hoja hiyo, Zitto alisema, kwa kuwa jambo hilo lilianzia bungeni wakati Mbunge wa Beatrice Shelukindo alipolieleza Bunge kuwa ana barua ya Jairo kuzitaka idara zichangie shilingi milioni 50 kila moja, wabunge walistahili kuijadili ripoti ya CAG kabla ya Serikali kufanya uamuzi.

Zitto alilieleza Bunge kuwa, kauli ya Luhanjo ni dharau kwa Waziri Mkuu, na imeingilia hadhi, kinga na madaraka ya Bunge kwa kuwa wabunge ndiyo wana mamlaka ya kuisimamia Serikali.

Zitto alipendekeza kwamba, shughuli na hoja zote za Serikali bungeni zisitishwe, kwanza wabunge waijadili taarifa za CAG kwa kuwa Bunge limepokwa nafasi yake.

Ndugai amewaeleza wabunge kuwa, Spika wa Bunge, Makinda, ataunda tume kuchunguza kudharauliwa kwa Bunge, na kukusanywa kwa fedha kwa ajili ya kupitishwa bajeti yaWizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2011/2012.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo wa Bunge tume hiyo itapaswa kufanya kazi haraka ili taarifa yake ijadiliwe katika mkutano ujao wa Bunge.
Chanzo: HabariLeo

Jairo awasha moto bungeni

Best Blogger Tips
BUNGE jana lilisitisha kwa muda shughuli zake za kawaida kujadili hatua ya Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo kumrejesha kazini Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo kabla ya Bunge kujadili Ripoti ya uchunguzi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Hatua hiyo imekuja siku moja baada ya Luhanjo kukutana na waandishi wa habari Dar es Salaam juzi na kuutangazia umma kwamba kutokana na matokeo ya uchunguzi huo kutomtia hatiani anaamuru Jairo arejee ofisini mara moja.

“Kutokana na matokeo haya ya uchunguzi wa awali, mimi kama Mamlaka ya Nidhamu ya Katibu Mkuu Nishati na Madini, sitaweza kuendelea na hatua ya pili ya kumpa taarifa ya tuhuma. Ninaamuru David Jairo arejee kazini kuanzia siku ya Jumatano.”

Hata hivyo, uamuzi huo wa Luhanjo jana uliamsha hasira za wabunge bila kujali itikadi zao za kisiasa ambao ambao walitaka Bunge lisitishe kujadili shughuli zozote kutokana na hatua hiyo ya Katibu Mkuu Kiongozi wakisema ni kudharau Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge.

Hoja ya Zitto

Hoja hiyo iliwasilishwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema) muda mfupi kabla ya kuanza kwa kipindi cha maswali na majibu. Zitto ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni alitoa hoja kutaka Bunge lisitishe kujadili hoja zote za Serikali hadi hapo ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali iliyomsafisha Jairo itakapofikishwa bungeni na kujadiliwa.

Zitto alianzisha moto huo mnamo saa 3:17 asubuhi ikiwa ni dakika moja tu baada ya Naibu Spika, Job Ndugai kutangaza taratibu za safari ya wabunge kwenda Zanzibar kwa ajili ya mazishi ya Mbunge Mussa Khamis Silima aliyefariki juzi.

Alitumia kanuni ya 51 kulieleza Bunge kuwa kitendo kilichofanywa na Luhanjo kilikiuka haki, maadili na madaraka ya Bunge na hivyo akataka wabunge wenzake wamuunge mkono ili wagome kufanya shughuli zozote za Serikali hadi hapo ripoti ya CAG kuhusu tuhuma dhidi ya Jairo itakapowasilishwa rasmi bungeni.

“Mheshimiwa Naibu Spika, jana kupitia vyombo vya habari tulimsikia Katibu Mkuu Kiongozi kupitia vyombo vya habari akieleza kuwa tuhuma zilizokuwa zikimkabili Jairo si za kweli na kwamba anatakiwa kurudi kazini kuanzia leo (jana),’’ alisema Zitto na kuongeza:

“Mheshimiwa Naibu Spika unafahamu ya kwamba, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alizungumza ndani ya Bunge hili ya kwamba angekuwa ni yeye angeshamchukulia hatua Ndugu Jairo kuhusu vitendo alivyofanya, hivyo basi naomba nitoe hoja kwamba Bunge lisitishe hoja yoyote ya Serikali mpaka itakapoleta bungeni taarifa ya CAG kuhusiana na uchunguzi huo.”

Baada ya kutoa hoja hiyo, Zitto aliungwa mkono na wabunge zaidi ya nusu waliokuwamo ndani ya ukumbi, hali ambayo ilimlazimisha Naibu Spika wa Bunge, Ndugai, kuitisha Kamati ya Uongozi kwa dharura kujadili suala hilo.

Hoja ya Lukuvi

Baada ya hoja ya Zitto, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisimama kupinga hoja hiyo akisema Mbunge huyo hakufuata taratibu zilizotakiwa ambazo ni kuwasilisha kusudio kabla ya kutoa hoja rasmi.

“Mheshimiwa Naibu Spika, najua jambo hili lina public interest (masilahi ya umma), lakini kanuni zinasema kuwa mbunge anayetaka kuwasilisha jambo lolote linalohusiana na shughuli za Bunge atafanya hivyo wakati unaofaa na uliowekwa na kanuni na atakuwa amemwarifu Spika mapema kuhusu kusudio lake, hivyo ulitakiwa kuwasilishiwa mapema ili uweze kuamua,’’ alisema Lukuvi.

Akijibu hoja hiyo, Ndugai alisema: “Wakati nasoma matangazo mbalimbali kuhusiana na kifo cha Mbunge, nilipata taarifa kutoka kwa Zitto kuhusu kunitaarifu juu ya jambo hilo, hivyo basi, hoja iliyotolewa na Zitto imetolewa kwa wakati na ilifuata utaratibu unaotakiwa.’’
Endelea kusoma habari hii.................

Sunday, August 21, 2011

Waasi wa Libya wathibiti mji wa Tripoli

Best Blogger Tips
Picha za televisheni zinaonyesha waasi katika uwanja wa Green Square katika mji mkuu, huku makundi ya watu wenye furaha wakisheherekea kuwasili kwa waasi hao katika uwanja huo.
Inaripotiwa waasi wamemkamata mwanawe Gaddafi Saif al-Islam, huku kiongozi mwenyewe akiahidi kuwa ataendelea kupigana.

Mwendesha mashtaka wa mahakama ya uhalifu wa kivita, Luis Moreno Ocampo amethibitisha Saif al-Islam, mwanawe Gaddafi, na ambaye alitarajiwa kumridhi babake amekamatwa.

Mwanawe wa kifungua mimba Mohammed Al Gaddafi naye amejisalimisha kwa waasi na anazuiliwa ndani ya makaazi moja mjini Tripoli.

Serikali ya Libya imesema takriban wanajeshi elfu 65 watiifu kwa kanali Gaddafi wamebakia mjini Tripoli lakini ni wachache tu walioonekana wakati waasi walipokuwa wakielekea kuuteka mji huo.

Mapigano yameripotiwa katika maeneo mengine ya mji. Mwandishi wa BBC mjini Tripoli amesema waasi wanajaribu kushika udhibiti wa jengo ambalo waandishi wa habari wako.

Inaaminika kuwa bado Kanali Gaddafi ana maelfu ya wafuasi waliojihami, japo ripoti zinaashiria kuwa idadi kubwa wamejisalimisha kwa waasi.

Msemaji wa serikali ya Libya , Moussa Ibrahim, amesema takriban watu 1300 wameuwawa mjini humo.

Awali Kanali Gaddafi aliwataka raia kujitokeza na kuukomboa mji wa Tripoli. '' Jitokezeni, jitokezeni niko nanyi. Msirudi nyuma. Tutapigana hadi kuikomboa nchi yetu kuzuia uthibiti. Msiwakubalie wanyakuzi kuiteka nchi yetu, nitapigana pamoja nayi kama nilivyoahidi'', Alisema Muammar Gaddafi.
Source: BBC

Saturday, August 20, 2011

Wapiganaji wa Libya wanajizatiti Zawiya

Best Blogger Tips
Wapiganaji wa Libya wanaendelea kusonga mbele kuelekea mji mkuu, Tripoli.

Televisheni ya wapiganaji hao imewaambia watu wajitayarishe kuwapokea.

Baada ya kuteka eneo la kati ya mji wa Zawiya, magharibi ya Tripoli, wapiganaji sasa wanasema wameiteka bandari muhimu ya Brega, mashariki mwa nchi, yenye kinu cha kusafisha mafuta.

Hakuna taarifa ya kuthibitisha hayo yanayotokea Brega.

Mwandishi wa BBC mjini Zawiya anasema kwenye medani wanayoiita medani ya mashujaa, katikati ya Zawiya, aliona majengo yaliyopigwa mabomu, yanayowaka moto, na kuta zenye matobo ya risasi.


Jana eneo hilo lilidhibitiwa kabisa na jeshi la Kanali Gaddafi.

Kulikuwa na mapigano makali jana jioni hadi usiku.

Lakini wapiganaji sasa wanaudhibiti mtaa, wamewatimua wanajeshi wa Gaddafi ambao wameelekea barabara ya kwenda Tripoli.

Kati ya medani alikuta maiti kama watatu.

Ameona maiti wanaoonesha kama Waafrika, na wapiganaji wanadai kuwa wanajeshi wengi wa Gaddafi ni askari mamluki kutoka kusini ya Sahara.

Ukweli hasa haujulikani, lakini maiti nyingi huko zinaonekana ni za Waafrika.

Sasa wapiganaji wanajitayarisha kusonga mashariki zaidi mwa mji, kuwatimua wanajeshi wa Gaddafi waliobaki Zawiya, ili kufungua njia ya kuelekea Tripoli.

Wapiganaji wa Libya wanadai kuwa waziri mkuu wa zamani, Abdessalem Jalloud, amekimbia Tripioli na amejificha katika maeneo yanayodhibitiwa na wapiganaji.
Source: BBC

Thursday, August 18, 2011

Simba, Simba utaipenda tu

Best Blogger Tips
Mshambuliaji wa Simba, Felix Sunzu Mumba akishangilia bao.
SIMBA, Simba ndio ulikuwa wimbo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam baada vijana hao wa mtaa wa Msimbazi kulipinza kisasi kwa ukifunga Yanga mabao 2-0 kwenye mchezo wa Ngao ya Jamii.

Simba waliofungwa kwenye Kombe la Kagame na Ngao ya Jamii mwaka jana vijana hao wa Mganda Moses Basena walizinduka na kupata mabao ya mapema kupitia kiungo Haruna Moshi 'Boban' dakika 15 na penalti ya Felix Sunzu dakika 38.

Simba iliyoanza kwa kasi mchezo huo ilifanikiwa kupata bao la kuongoza kupitia kwa Moshi 'Boban' aliyemalizia vizuri krosi ya kutoka upande wa kushoto iliyopigwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Sunzu aliyekuwa na ushirikiano mkubwa na Emmanuel Okwi.

Mshambuliaji Sunzu alifungia Simba bao la pili kwa mkwaju wa penalti baada ya Nadir Haroub kumchezea vibaya Moshi 'Boban', kwenye eneo la hatari dakika 35. Sunzu alilazimika kuonyesha ueledi wake pale alipotakiwa kurudia penalti hiyo baada ya mwamuzi Israel Mjuni kusema Kado alitokea kabla ya kupigwa kwa penalti ya kwanza pamoja na kuwa alikuwa amefunga.

Kocha Moses Basena aliyeonekana kujifunza kwa makosa alitumia mfumo wa 4:2:3:1 na kutoa nafasi kubwa kwa Okwi, Haruna na Sunzu kutawala sehemu kubwa ya kiungo tofauti na ilivyokuwa kwenye fainali ya Kombe la Kagame.

Okwi alifanya atakalo mbele ya mabeki wa Yanga walionekana kuwa kama watu waliozidiwa na mazoezi na kukosa unyumbulifu mchezoni, huku safu ya ulinzi wa Simba chini ya mkongwe Victor Costa aliweza kuwapoteza mchezoni kabisa mshambuliaji Keneth Asamoah na Jerry Tegete.

Kiungo Haruna Niyonzima alijitahidi kuonyesha uwezo mkubwa wa kutawala mpira na kujaribu kutafuta goli kwenye mechi yake ya kwanza ya watani wa jadi, lakini alikosa msahada kutoka kwa wenzake.

Simba ilianza mashambulizi kwa kasi na dakika kwanza Okwi alikosa bao baada ya shuti lake kumgonga Haroub na kupaa juu ya goli.

Okwi alipoteza nafasi nyingine dakika 8 baada ya kuwalamba chenga mabeki wa Yanga, lakini aliugonga mpira mbele zaidi na kipa Shaaban Kado akauwahi.

Beki wa Yanga, Chacha Marwa, nahodha Shadrack Nsajigwa alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Okwi. Naye Juma Nyoso wa Simba alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Asamoah.

Haruna Niyonzima alipiga shuti la umbali wa mita 25 baada ya kumchungulia Juma Kaseja kwa bahati mpira huo ulipaa juu ya goli.

Kipindi cha pili Yanga iliamka baada ya kuingia Hamisi Kiiza na Rashid Gumbo lakini walishindwa kuipenya ngome ya Simba.

Yanga waliendeleza sera yao ya kugomea jezi za wadhamini wa ligi Vodacom zenye nembo nyekundu kwa kuvaaa jezi za mdhamini wao TBL tofauti na Simba wenyewe walivaa zile walizopewa na Vodacom

Vikosi Yanga; Shaaban Kado, Shadrack Nsajigwa, Oscar Joshua, Nadir Haroub, Chacha Marwa, Juma Seif, Godfey Taita, Haruna Niyonzima, Keneth Asamoah/ Gumbo, Jerry Tegete, Kigi Makasi/ Kiiza.

Simba: Juma Kaseja, Said Nasoro, Amir Maftah, Juma Nyoso, Victor Costa, Partick Mafisango,  Salum Machaku/ Kiemba, Jerry Santo, Felix Sunzu, Haruna Moshi/ Gervais Kago, Emmanuel Okwi/ Kapombe.
Source: Mwananchi

Monday, August 15, 2011

‘ Kutumia gesi kwenye gari Sh1 milioni’

Best Blogger Tips
WIZARA ya Nishati na Madini imesema zaidi ya Sh1 milioni zinahitajika kwa ajili ya kubadilisha mfumo wa gari moja linalotumia mafuta ya petroli kutumia gesi asilia, Bunge lilielezwa jana.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Adam Malima aliliambia Bunge hayo jana wakati akijibu swali la Mbunge wa Muheza (CCM) Herbert Mtangi aliyetaka kujua Serikali inasema nini kuhusu utekelezaji wa mradi wa gesi kwa magari hapa nchini.

Waziri Malima alisema mpaka sasa mifumo ya magari 36 yamebadilishwa ili kuweza kutumia gesi asilia ambapo alisema kasi ya ubadilishwaji wa mifumo ya magari ni ndogo kutokana na gharama za ubadilishaji kuwa kubwa.

Aidha Malima alisema kasi ndogo ya za elimu juu ya suala hilo imesababisha  ufahamu mdogo wa manufaa ya matumizi ya gesi kwenye magari ikilinganishwa na matumizi ya petroli.Alifafanua kuwa mkakati wa Serikali wa awali mwaka 2008, ulikuwa ni kuanzisha vituo vya mfano na masoko ambapo walianzisha kituo cha kujaza gesi kwenye magari  ubungo.

Alisema kituo hicho kina uwezo wa kujaza magari 200 kwa siku.
Alisema Serikali kupitia TPDC kwa kushirikiana na Pan African Energy walianza mchakato wa mradi wa kutumia gesi asilia kwenye magari, viwandani pamoja na majumbani kwa lengo la kupanua manufaa ya kiuchumi na kijamii.
Source: Mwananchi

Saturday, August 13, 2011

Kikwete aongoza maziko ya Mayunga

Best Blogger Tips
RAIS Jakaya Kikwete ameongoza mamia ya waombolezaji kumzika Luteni Jenerali (mst) Silas Mayunga kwenye makaburi ya Wasabato ya Unyanyembe mjini hapa.

Jenerali Mayunga, shujaa wa Operesheni Chakaza ya kumng’oa Iddi Amin baada ya kuwa ameivamia Tanzania mwaka 1978, alifariki dunia mwishoni mwa wiki iliyopita katika Hospitali ya Apollo jijini New Delhi, India, ambako alikuwa anatibiwa.

Alikuwa na umri wa miaka 71.

Jenerali Mayunga alizikwa juzi kwa taratibu zote za Kanisa la Wasabato na za kijeshi ikiwa ni pamoja na kupigiwa mizinga 15 na gwaride la heshima la Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Rais Kikwete aliungana na viongozi wa kitaifa katika maziko hayo ambao ni pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Edward Lowassa ambaye ni Waziri Mkuu wa zamani na Waziri wa Ulinzi Hussein Mwinyi.

Wengine ni Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Amina Masenza, wenyeviti wa CCM wa mikoa ya Shinyanga na Mwanza, wabunge wa Mkoa Shinyanga akiwamo Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge, Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Davies Mwamunyange na viongozi wengine waandamizi wa Jeshi na wapiganaji.

Rais Kikwete akifuatana na mkewe Mama Salma, aliwasili makaburini saa 9.56 alasiri akitokea Dar es Salaam ambapo pia alikuwa na ziara ya siku mbili Shinyanga ikiwa ni pamoja na kuhudhuria maziko hayo.

Mara baada ya Rais kuwasili makaburini, gwaride la Jeshi lililobeba mwili wa marehemu, liliingia eneo la makaburi saa 10.12 jioni na mwili wa marehemu kuteremshwa kaburini saa 10.30.

Mjane wa marehemu na watoto wake walikuwa wa kwanza kuweka udongo kaburini wakifuatiwa na Rais na Mama Salma, Lowassa, Mwinyi, Masenza, Jenerali Mwamunyange na Naibu Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Uganda, Luteni Jenerali Colleta Ivan, ambaye baadaye
aliwasomea waombolezaji salamu za rambirambi za Rais Yoweri Museveni.

Katika salamu zake, Rais Museveni alielezea mchango wa Jenerali Mayunga katika Operesheni Chakaza akisema alikuwa Jenerali ambaye alimpokea Museveni na wapiganaji wake 28 wa awali kwenye Shule ya Msingi ya Nyamiyanga mkoani Kagera Desemba 23, 1978.

Alisema: “Wakati Kampala inatekwa kutoka mikononi mwa majeshi ya Iddi Amin na kufikia hatua muhimu ya kuikomboa Uganda Aprili 11, 1979, askari wapiganaji katika kikosi hicho cha Waganda walikuwa 9,000 na yote hii ilikuwa kazi ya Jenerali Mayunga ambaye alitoa
mchango mkubwa sana kuongeza askari hao kwa kiwango hicho kikubwa. Tumepotelewa na mpiganaji na Kamanda hodari.”
Source: HabariLeo
 

Wednesday, August 10, 2011

Ripoti ya kunyanyaswa watoto Tanzania

Best Blogger Tips
Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na shirika linaloshughulikia maslahi ya watoto la UNICEF karibu theluthi moja ya watoto wa kike nchini Tanzania wanakabiliwa na unyanyasaji wa kijinsia na kuingiliwa bila hiari kabla hawajatimia umri wa miaka 18.

Shirika hilo linasema kuwa watoto wa kiume idadi yao inafika asili mia 13.4.

Kinachotumika sana katika unyanyasaji huu ni kuwatomasa watoto ambako baadae hufuatiwa na jaribio lakutaka kuwaingilia.

Afisa mmoja wa shirika hilo Andy Brooks amesema uchunguzi huu ndio uliokamilika zaidi na umeonesha kuwa serikali iko tayari kukabiliana na tatizo hili.

Uchunguzi huu pia uligundua kuwa wale ambao wamejihusisha na mapenzi kabla ya kutimia umri wa miaka 18, asili mia 29.1 ya watoto wa kike na asili mia 17.5 ya wale wa kiume wamesema kuwa mara ya kwanza wao kujihusisha na ngono haikuwa kwa hiari yao.

Unicef inasema hii ina maana walilazimishwa ama kushawishiwa kujihusisha na ngono.

Waziri wa Elimu wa Tanzania Shukuru Kawambwa amesema kuwa serikali imejitolea kukomesha unyanyasaji wa kijinsia na kuingiliwa watoto.

Bw Brooks amesema uchunguzi sawa na huo utafanywa nchini Kenya, Rwanda, Malawi, Zimbabwe na Afrika Kusini.
Source: BBC

Sunday, August 7, 2011

Kondoo mwenye Korani azaliwa

Best Blogger Tips
Via HabariLeo

KIJIJI cha Uduru wilayani Hai mkoani Kilimanjaro kimegeuka eneo la utalii baada ya waumini wa madhehebu ya Kiislamu kutoka maeneo mbalimbali wilayani humo na maeneo jirani, kwenda kumshuhudia kondoo aliyezaliwa ameandikwa maneno mwilini kwa lugha ya Kiarabu.

Waumini hao walifurika kijijini hapo juzi baada ya sala ya Ijumaa kumshuhudia kondoo huyo aliyezaliwa wiki tatu zilizopita na kuacha watu midomo wazi kutokana na kuwa na maandishi yanayosomeka kiarabu ubavuni, yakitafsiriwa kwa Kiswahili kama Yasini.

Kondoo huyo aliyezaliwa katika familia moja ya waumini wa dini ya Kikristo, aliwavuta
waumini wengi kijijini hapo na kutoka nje ya wilaya na mkoa wa Kilimanjaro kwa ajili ya kushuhudia tukio hilo la ajabu na la kihistoria ambalo halijawahi kutokea.

Akizungumza na HABARILEO Jumapili kijijini hapo, mmiliki wa kondoo huyo, Grace
Massawe (55) alisema kondoo huyo alizaliwa takribani wiki tatu zilizopita na hakuwahi kutambua kwamba beberu huyo alikuwa na maandishi hayo, kutokana na kutotolewa nje na mama yake.

Grace alisema baada ya kondoo huyo kuzaliwa, mama yake alibadilisha tabia na kukaa ndani ambapo awali alikuwa akila chakula nje na wenzake, lakini aligundua maandishi hayo baada ya kumtoa nje mwenyewe.

Alisema awali aliona herufi ya W yenye rangi ya dhahabu, lakini siku zilivyozidi kwenda neno hilo lilizidi kukua na kubadilika rangi na kuwa jeupe zaidi, hali iliyompa wasiwasi na kutafuta msaada ili kutambua maana ya maandishi hayo kutoka kwa waumini wa Kiislamu.

“Baada ya waumini wa Kiislamu kufika hapa nyumbani walibaini maandishi hayo ubavuni mwa kondoo huyo kuwa ya Kiarabu yanayosomeka kuwa Yasini,” alisema Grace.

Alisema waumini hao walimweleza kuwa neno hilo ni muhimu sana katika Kitabu Kitakatifu cha Korani, ambalo ni kama kitovu cha kitabu hicho, pia ni moja ya sura muhimu ndani ya kitabu hicho.

Katika hatua nyingine, Grace alisema katika ufugaji wake wa kondoo hakujawahi kutokea tukio la ajabu kama hilo na kueleza kuwa kondoo aliyemzaa alikuwa ni uzao wake wa mara ya pili ambapo awali alizaa kondoo wa kawaida.

Alisema kutokana na kondoo huyo kuvuta hisia za watu wengi, pia viongozi wakubwa wa dini hiyo walifika kushuhudia maajabu hayo, akiwamo Katibu wa Baraza Kuu la Waislamu
Tanzania (Bakwata) wa Mkoa wa Kilimanjaro, Shehe Rashid Mallya, na Shehe Mkuu wa Wilaya ya Hai, Juma Lyimo.

Baadhi ya waumini waliofika kumshuhudia kondoo huyo na kuzungumza na gazeti hili Aman Ramadhan na Yacoub Mushi wa Lyamungo, walisema tukio hilo ni muujiza wa Mungu uliojitokeza, hususan kipindi hiki cha mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Juhudi za kumtafuta Shehe Mallya kuzungumzia tukio hilo, zilishindikana baada ya simu yake kuita bila kupokewa.

Saturday, August 6, 2011

Itibari ya Marekani inapungua

Best Blogger Tips
Vyombo vya habari vya Uchina vimeilaumu vikali Marekani, baada ya itibari ya Marekani kama mkopaji kushushwa kutoka kiwango cha juu kabisa cha A tatu na kampuni moja inayotoa vipimo hivyo ya Standard and Poor's.

Shirika la habari la taifa la Uchina, Xinhua, lilisema siku za Marekani kuweza kukopa tu ili kuziba upungufu wake, zimekwisha.

Na lilitaka Marekani kuhakikisha kuwa pesa ambazo Uchina imeikopesha Marekani ni salama.
Mchambuzi wa maswala ya uchumi mjini Hong Kong - Francis Lun, Meneja Mkurugenzi wa Lyncean Holdings - anasema hayo yaliyotokea Marekani ni hasara kubwa kwa Uchina na Japani.

"Kwa kupunguziwa hadhi ya uwezo wa Marekani kulipa madeni yake, ina maana kiwango cha riba lazima kipande, kwa sababu mikopo ya Marekani sasa ni A-mbili na ushee, siyo A-tatu.

Serikali ya Marekani itabidi kulipa riba zaidi juu ya mkopo wa taifa, na hivo inamaanisha kuwa kiwango cha riba kikipanda, sehemu ya mkopo wenyewe inapungua.

Uchina imeikopesha serikali ya Marekani dola trilioni moja pointi moja.

Japani imeikopesha dola trilioni moja, na ikiwa bei itapungua kwa asili mia moja tu, basi Uchina itapoteza dola bilioni 11; na Japani itapata hasara ya dola bilioni 10 mara moja."
Soource: BBC

Thursday, August 4, 2011

Kikombe cha Babu chashindwa kutibu ukimwi

Best Blogger Tips
  • Waliokunywa wapimwa baada ya siku 90
  • Matokeo yaonyesha bado wana virusi
  • Wailaumu Serikali ‘kubariki’ kikombe cha Babu
MACHI 20 mwaka huu, Mwenyekiti wa Mtandao wa Watu Wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (TANOPHA+), Julius Kaaya alikuwa safarini na wenzake 14 wanaoishi na virusi hivyo kwenda kijiji cha Samunge, wilayani Ngorongoro, kupata tiba ya “kikombe” cha Mchungaji Ambilikile Masapila; maarufu kwa jina la Babu wa Loliondo.

Kaaya na wenzake walikuwa na imani kubwa kuwa huenda tiba hiyo ikawa ndiyo mwisho wa mateso na mahangaiko ya muda mrefu yanayotokana na kusumbuliwa na virusi vya ugonjwa huo hatari ambao hadi sasa dunia haijapata tiba yake.

Watu hao walikuwa wamesafirishwa kwa msaada wa shirika la (EACNASO) ambalo pia ni muungano wa mtandao wa mashirika yanayojishughulisha na ugonjwa huo kwa nchi za Afrika ya Mashariki lenye makao yake mjini Arusha.

Imani ya waathirika hao ilijengwa juu ya msingi kuwa dawa ya kikombe cha Babu kwa wakati huo ilikuwa gumzo kubwa nchini na viongozi mbalimbali wa serikali kutoka kada mbalimbali, kama mawaziri wa serikali, majaji wa Mahakama Kuu, wenyeviti wa vyama vya siasa, wakuu wa mjeshi na wananchi, walipigana vikumbo katika kijiji hicho kupata uponyaji wa maradhi yanayowasumbua kupitia tiba hiyo.

Baada ya safari ngumu ya siku moja na nusu kutokana na ubovu wa barabara, Kaaya na wenzake walifika Samunge na kupata tiba ya kikombe cha Babu; huku wakipewa siku 90 kama muda ambao virusi vitakuwa vimetoweka katika miili yao.

Aidha, majibu ya vipimo vya watu hao pia vilikuwa vinasubiriwa kwa hamu na makundi mbalimbali katika jamii kutokana na watu hao kujitangaza kuishi na virusi hivyo na kuwa tayari kuweka hadharani majibu ya vipimo vya hali zao.

Lakini miezi minne sasa tangu muda uliotolewa “kisayansi” na Mchungaji Masapila kuwa virusi vitakuwa vimeisha miilini mwao, Kaaya na wenzake wote waliotumia tiba hiyo wamevunjika moyo baada ya kupimwa upya na kuonekana kuwa bado wana virusi vya ugonjwa huo hatari.
Endelea kusoma habari hii......................

Wednesday, August 3, 2011

Treni mpya ya kasi yaanza Afrika Kusini

Best Blogger Tips
Gautrain
Treni iendayo kasi barani Afrika, imeanza safari yake mpya kuelekea mji mkuu, Pretoria, kutoka Johannesburg katika jitahada za kurahisisha usafiri baina ya miji hiyo mikubwa ya Afrika Kusini.

Treni hiyo ijulikanayo kwa Gautrain inachukua chini ya dakika thelathini kwa safari ya umbali huo wa kilometa 54.

Kwa gari mwendo wa safari hiyo huchukua hadi saa mbili wakati watu wengi wakiwa wanatumia usafiri kwenda ama kurejea kazini.

Safari ya treni hiyo ya Gautrain kwa njia ya kueleka uwanja wa ndege ilizinduliwa wakati wa mashindano ya Kombe la Dunia mwaka 2010, ambapo maelfu ya mashabiki wa soka waliitumia kusafiria.

Lakini kwa kufika Pretoria, inaonekana itatumia zaidi na wasafiri wa kawaida nchini Afrika Kusini ili kukabiliana na foleni katika barabara yenye magari mengi nchini humo.

Mamia ya watu walimiminika katika kituo cha treni cha Rosebank mjini Johannedburg tangu mapema saa kumi na moja na nusu alfajiri kuwahi treni ya kwanza iliyoelekea Pretoria.

Kulikuwa na matatizo kidogo yalijitokeza, ikiwemo matatizo ya kiufundi katika behewa moja, lakini wahandisi wamesharekebisha tatizo hilo, kwa mujibu wa maafisa wa Gautrain.

Serikali imesema lengo lake ni kuufanya usafiri wa treni ndio uti wa mgongo wa mfumo wa usafiri wa umma, kwa mujibu wa Waziri wa Usafiri, Sbu Ndebele.

Treni hiyo ya Gautrain imegharimu randi bilioni 24 sawa na dola bilioni 3 kuijenga.

Kasi ya treni hiyo ni kilometa 160 kwa saa.

Gautrain inatarajiwa kupunguza idadi ya magari katika barabara ya N1 Ben Schoeman inayounganisha Pretoria na mji wa kibiashara wa Afrika Kusini wa Johannesburg kwa asilimia 20.
Source: BBC

Monday, August 1, 2011

Muafaka kuhusu deni la marekani

Best Blogger Tips
Rais Barack Obama
Rais Barack Obama ametangaza kuwa viongozi wa chama cha Republican na chake cha Democratic wameafikiana kuhusu mpango wa kulipia deni la serikali.

Bw Obama amesema chini ya makubaliano hayo nchi hiyo itapunguza matumizi yake kwa dollar trilioni moja katika kipindi cha miaka kumi ijayo.

Hata hivyo mpango huo utapigiwa kura kwenye baraza za senate hii leo.

Muafaka huo umefikiwa ikiwa imebakia siku moja tuu kabla ya makataa ya kuongeza kiwango cha kukopa fedha za kulipia madeni yake.

Kwa wiki kadhaa, viongozi wa vyama hivyo wamekuwa wakivutana kuhusu njia bora ya kufuata kukabili madeni ya marekani.

Hali ambayo ilitishia kukwamihsa shughuli za serikali.

Baraza la senate lina hadi kesho kupiga kura kuongeza kiwango hicho cha kukopa hadi dola trilioni 14 lau sivyo shughuli za serikali zitakwama.

Rais Obama amesema kuwa mpango ulioafikiwa sio ule aliotarajia lakini amelazimika kuukubali ilikuwezesha huduma za serikali kuendelea na madeni yake yalipwe.

Utawala wa Rais Obama ulikuwa unakabiliwa na shinikizo kali kutoka kwa wapinzani kutoka chama cha Republican ambao walikuwa wanapinga pendekezo lake la kuwepo na mpango ambao utasitiri hali hadi mwisho wa mwaka ujao.

Chama cha Republicans kilitaka mpango huo uwepo hadi katikati ya mwaka ujao. Lakini sasa vyama hivyo vimekubaliana kuunda kamati maalum itakayotoa mapendekezo mapya mwezi Novemba.

Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits