Tuesday, September 18, 2012

Madaktari waliogoma waiangukia serikali

Best Blogger Tips
MADAKTARI waliokuwa kwenye mafunzo kwa vitendo ambao Serikali iliwafutia vibali vya kazi, wamesalimu amri na kuamua kumuangukia aliyekuwa mwajiri wao ili awarudishe kazini.

Serikali iliwafukuza kazi madaktari hao baada ya kutangaza mgomo usio na kikomo Juni mwaka huu, hadi madai yao yatakapofanyiwa kazi ambapo mgomo huo ulisababisha vifo kwa baadhi ya wagonjwa waliokosa huduma za matibabu.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari walioathirika na mgomo, Bw. Paul Swakala, alisema wameamua kuomba msamaha kwa Rais Jakaya Kikwete na Watanzania wote baada ya kubaini kuwa, wagonjwa wengi waliathirika na mgomo huo.

Alisema walishindwa kuuepuka mgomo huo kutokana na mazingira ya wao kufanya kazi na Madaktari Bingwa kwani mikataba yao, haikuwaruhusu kufanya kazi ya kutoa matibabu peke yao.

“Tunafahamu kuwa, Watanzania wengi waliathirika mgomo ule, tunawaomba radhi sana kwa usumbufu walioupata na tunakiri kuwa kila mmoja wao alichokizwa na uamuzi wetu.

“Japo nchini kwetu utamaduni wa kuomba radhi hadharani haupo, sisi tumeamua kufanya hivi kwa sababu tumekosa na hakuna binadamu aliye kamili wote tunakasoro,” alisema Bw. Swakala.

Aliongeza kuwa, wanatambua na kuunga mkono juhudi za Rais Kikwete katika kuboresha huduma za afya nchini licha ta changamoto nyingi zinazoikabili sekta hiyo.

“Tunamuomba radhi sana Rais Kikwete na Serikali yake kwa usumbufu uliosababishwa na mgomo, pia tunatambua jitihada zake za kutafuta suluhu ya mgomo uliopo,” alisema.

Aliwahakikishia Watanzania kuwa, kuanzia sasa hawako tayari kushiriki mgomo kwa namna yoyote kwabni kufanya hivyo ni kuweka rehani maisha ya wagonjwa.

Bw. Swakala alisema wanajutia kosa hilo na wako tayari kulejea kazini ili kuwahudumia Watanzania kwa moyo mweupe na wanayo dhamira ya kounana na Rais Kikwete ana kwa ana ili kumuomba radhi.

Akijibu maswali ya waandishi wa habari, Bw. Swakala alisema madaktari ambao wamesaini fomu za kuomba radhi ni 200 kati ya 364 waliofutiwa vibali vya kazi.

“Mimi nimesoma kwa gharama za sh. milioni 35, sioni faida ya kukaa mtaani wakati Watanzania wakiendelea kupata  shida ya matibabu,” alisema Bw. Swakala.

Akizungumzia suala la vifaa ambalo ni moja ya sababu iliyowafanya wagome, Bw. Swakala, wao wanaamini Rais Kikwete na Serikali yake itaboresha mazingira ya huduma za afya.

“Chama cha Madaktari nchini (MAT) ni cha hiari, hatuungani na msimamo wao, wanachama walionao ni madaktari wenye usajili wa kudumu si kama sisi, hatulazimishwi kujiunga nao,” alisema.

Madaktari hao walifanya mgomo huo ili kuishawishi Serikali iboreshe mazingira ya kazi, nyongeza ya mishahara na marupurupu mengine.
Source: Tanzania Daima

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits