Saturday, June 30, 2012

Morsi akabidhiwa madaraka na Tantawi

Best Blogger Tips
 Rais wa kwanza wa kiraia wa Misri, na kutoka chama cha Kiislamu, Mohammed Morsi, ameapishwa, na ametoa wito kuwa bunge la nchi lirejeshwe haraka - bunge lilofutwa hivi karibuni.

Katika sherehe kwenye eneo la jeshi nje ya Cairo, kiongozi wa wakuu wa jeshi wanaoongoza nchi, Field Marshal Mohammed Tantawi, alikabidhi madaraka rasmi kwa Rais Morsi.

Hapo awali, akitoa hotuba yake ya kwanza iliyogusia mambo mengi, katika Chuo Kikuu cha Cairo, Bwana Morsi alisema atalilinda jeshi kama taasisi, lakini piya alionya jeshi halifai kuwa mbadala wa matakwa ya wananchi.

Bwana Morsi aliahidi ukurasa mpya utaong'ara katika historia ya nchi, kufwatilia ule aliosema ni ukurasa wa kuchusha.

Alipokuwa akizungumza, akina mama ambao watoto wao waliuliwa chini ya utawala wa Rais Mubarak, walibeba juu picha za watoto wao hao wa kiume.

Bwana Morsi piya alisema Misri haitotapakaza mapinduzi nchi za nje.

Rais mpya aliapishwa kwenye sherehe iliyofanywa katika mahakama ya katiba mjini Cairo.
Chanzo: BBC

Friday, June 29, 2012

Daktari: Hali ya Ulimboka mbaya

Best Blogger Tips
 AFYA ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk Steven Ulimboka imebadilika na kuwa mbaya, baada ya figo zake kushindwa kufanya kazi ya kuchuja sumu ya mwili na kusababisha apatiwe huduma ya kusafisha damu yake.

Habari zilizopatikana jana na kuthibitishwa na kiongozi wa jopo la madaktari wanaoendelea kumtibu, Profesa Joseph Kahamba, zilieleza kuwa hali ya Dk Ulimboka ilibadilika na kuwa mbaya na hivyo kuwapo mikakati wa madaktari wenzake kukusanya fedha ili kumpeleka nje ya nchi.

Dk Ulimboka ambaye amelazwa katika Kitengo cha Wagonjwa Wanaohitaji Uangalizi Maalumu (ICU) katika Taasisi ya Mifupa (MOI), alipatiwa huduma hiyo jana asubuhi kwa kutumia mashine maalumu, iliyoko katika Kitengo cha Watoto cha Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).

Daktari huyo ambaye alikuwa anaratibu mgomo wa madaktari unaoendelea nchi nzima kutokana na Serikali kushindwa kutimiza madai yao mbalimbali, amelazwa kutokana na majereha aliyoyapata katika sehemu mbalimbali za mwili, baada ya kutekwa na watu wasiojulikana, kisha kupigwa, kung'olewa kucha, meno mawili na kutupwa katika Msitu wa Pande, usiku wa kuamkia Jumatano.

Tangu alazwe MOI baada ya kuokotwa na wasamalia wema, katika Msitu wa Pande uliopo nje kidogo ya Jiji la Dares Salaam, hali ya afya ya Dk Ulimboka imekuwa tete na jana ilizidi kuwa mbaya.

Kauli ya Dk Kahamba

Akizungumza na gazeti hili jana, Profesa Kahamba alisema kutokana na tatizo hilo, mgonjwa huyo jana alilazimika kusafishwa damu.

Alieleza hayo alipotakiwa kuthibitisha taarifa zilizolifikia gazeti hili kuwa afya ya Dk Ulimboka haikuwa nzuri na madaktari wanachangishana fedha kumpeleka kwenye matatibu ya kusafishwa damu katika Hospitali ya Regency jijini Dar es Salaam au nje ya nchi.

"Taarifa hizo zina ukweli, lakini siyo jambo rahisi kiasi hicho kwamba anatakiwa kusafishwa damu. Kama ni damu amesafishwa leo (jana) asubuhi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili," alisema Profesa Kahamba na kuendelea:

"Suala lake ni complicated (tata) zaidi, lakini ili watu waelewe, siyo mbaya mkisema figo zimefeli(zimeshindwa kufanya kazi)."

Alipotakiwa kueleza sababu ya tatizo hilo, Profesa Kahamba alisema, "Siwezi kueleza kwa undani ila haya maumivu ya kupigwa na kuteswa yanachangia kwa kiasi kikubwa."

Alipotakiwa kueleza yeye anaonaje hali ya sasa ya Dk Ulimboka, Profesa Kahamba alisema: “Ni uongo tukisema anaendelea vizuri."

Aliendelea, "Unajua alipofikishwa hapa Muhimbili juzi (Jumatano) afya yake ilikuwa mbaya, na jana (Alhamisi) alionekana kuendelea vizuri, lakini jana hiyohiyo, hali yake ilianza kubadilika na vipimo vilionyesha kuwa ana complications (matatizo) za figo.

"Sasa figo ni kitu sensitive (muhimu) sana, anahitaji uangalizi wa karibu na kimsingi hatuwezi kusema kwamba anaendelea vizuri. Ni vyema tukisema tu afya yake ni mbaya," alieleza.

Taarifa za awali kutoka kwenye chanzo chetu hospitalini hapo, zilieleza kuwa Dk Ulimboka ambaye alipata tatizo linalojulikana kama “Acute renal failure”, alifanyiwa tiba inayojulikana kama Dialysis, ambayo ni kitendo kutumia mashine maalumu kufanya kazi ya kuchuja sumu ya mwili kwenda kwenye mkojo, baada ya figo ambazo hufanya kazi hiyo kushindwa.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, Dialysis inaweza kumsadia mgonjwa ambaye figo zake zimeshindwa kufanya kazi, kuishi kama kawaida, lakini kwa Dk Ulimboka haikutoa matokeo mazuri.

Michango ya madaktari


Jana ulifanyika Mkutano wa Madaktari Bingwa wa MNH, Chuo Kikuu Sayansi ya Tiba Muhimbili (MUHAS) na Ocean Road (ORCI) na kuazimia kukusanya Dola za Marekani 40,000 (Sh64,000,000) ili Dk Ulimboka asafirishwe kwenda India kwa matibabu zaidi.

Taarifa za maazimio hayo zilitangazwa kwa waandishi wa habari na Katibu wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Edwin Chitega, kuwa afya ya Dk Ulimboka haikuwa nzuri hivyo zikipatikana fedha hizo angepelekwa nje ya nchi.

Dk Chitega aliwataka wanataaluma hao na wananchi kwa ujumla kuchangia safari hiyo ili kuokoa maisha ya daktari huyo, huku akitaja namba za mawakala wa simu za Vodacom na Tigo, ambazo zitatumika kukusanya michango hiyo.

Habari zilizopatikana baadaye wakati tunakwenda mitamboni zilieleza kuwa, Dk Ulimboka alitarajiwa kusafirishwa kwenda Nairobi, Kenya kwa matibabu zaidi.


TANNA MOI watoa tamko
Katika hatua nyingine, Chama cha Wauguzi (Tanna), Tawi la MOI kilitoa tamko la kulaani kitendo cha kutekwa, kupigwa na kujeruhiwa kwa Dk Ulimboka na kutaka uchunguzi wa kina na haraka ufanyike ili kubaini watu waliohusika.

Mwenyekiti wa Tanna, Tawi la Moi, Prisca Tarimo alisema katika tamko hilo kuwa, kitendo alichofanyiwa Dk Ulimboka ni cha kinyama na kisicho cha kiutu.

Katika tamko hilo, Tanna imeomba Serikali kutafuta suluhu ya mgomo huo haraka kwa kuwa unaathiri maisha ya watu na kuwaongezea mzigo wa kiutendaji wauguzi.

Mgomo wa madakati unaingia siku ya saba leo, huku suluhu ya kuaminika ya kutatua tatizo hilo, ikiwa bado haijapatikana.

Polisi wakanusha
Katika hatua nyingine, James Magai anaripoti kuwa, Jeshi la Polisi limekanusha kumteka na kumjeruhi Dk Ulimboka, huku likipinga pia taarifa za daktari huyo kumtambua mmoja wa askari walio katika jopo la uchunguzi wa tukilo hilo alipokwenda kumtembelea hospitalini.

Pia jeshi hilo limetoa wito kwa madaktari hao walioko katika mgomo kuwa na busara na kutii amri ya Mahakama, ya kuwataka wasitishe mgomo wao.

Pia limeonya kuwa ikiwa wataendelea kukaidi na kupuuza amri ya hiyo ya mahakama, linao wajibu wa kuwachukulia hatua kwa kuwafikisha mahakamani, ili wajibu mashtaka hayo.

Msimamo huo ulitolewa jana na Kamishna wa Oparesheni Maalumu, Kamishna wa Polisi (CP), Paul Chagonja wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari kwenye mkutano alioitisha kuzungumzia matokeo ya operesheni ya jeshi hilo ya majuma matatu katika kuzuia uhalifu nchini.

Alisema madai hayo ni uvumi ambao unalenga kulifanya jeshi hilo lisiaminike na kufifisha juhudi zake za kuwasaka waliohusika na unyama huo.
Chanzo: Mwananchi

Thursday, June 28, 2012

Dkt. Ulimboka akiwa Hospitalini

Best Blogger Tips




Source: Wavuti




Madaktari 72 watimuliwa kazi Mbeya

Best Blogger Tips
 BODI ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya, imewasimamisha kazi
madaktari 72 kwa kosa la kutoingia kazini kwa siku tano jambo ambalo
ni kinyume cha makubaliano ya mkataba.


Imeelezwa kuwa madaktari hao ambao 54 ni wale wa mafunzo ambao
waliingia mkataba wa miaka miwili na hospitali ya Rufaa na madaktari
18 ni wale walioajiriwa na Wizara ya afya.


Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Bodi Kaimu Mkuu wa
Mkoa wa Mbeya Norman Sigara, alisema kitendo cha madaktari kutoripoti
kazini kwa siku tano ni ukiukwaji wa kanuni za utumisha wa umma toleo
la 2009 kifungu namba F.16-F17 na F. 27.


"Hivyo kupitia kanuni hiyo madaktari hao wamesimamishwa kazi na
kurudishwa kwa mwajiri wao ambaye ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya na
Ustawi wa Jamii kwa hatua zaidi za kinidhamu,"alisema Sigara.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo wa Bodi, imeelezwa kuwa siku ya tarehe
23/6/2012 wafanyakazi 15 waliokuwa zamu(Intern Doctors 12 na
Registrars3) hawakufika kazini na tarehe 24/6/2012 wafanyakazi
19(Intern doctors 15 na Registrars 4) hawakufika kazini.


Alisema, kuanzia tarehe 25/6/2012 hadi leo imethibitika kuwa Interns
doctor 54 na Registrars 18 hawakufika kazini hadi leo tarehe 28/6/2012
ambapo tarehe 25/6/2012 bodi ya hospitali ilifanya kikao cha dharura
kujadili hali ya utendaji kazi na utoaji huduma hospitalini na kutoa
uamuzi.


Sigara, aliyataja maamuzi hayo kuwa ni Mwenyekiti wa Bodi akutane na
madaktari ambao hawakufika kazini ili awasikilize sababu za kutofika
na kujadili namna ya kumaliza matatizo hayo jambo ambalo madaktari hao
waligoma.


Alisema, baada ya madaktari hao kukaidi ombi hilo, Bodi ya hospitali
ili waandikia barua za kujieleza kwanini wasichukuliwe hatua za
kinidhamu kwa kuvunja mkataba walioingia na hospitali na pia kukiuka
kanuni za kudumu za utumishi wa umma nalo walilikaidi

"Iwapo madaktari ambao hawakuripoti au kueleza sababu za kuridhisha
ifikapo tarehe 28/6/2012. Kwa kuzingatia kanuni za utumishi wa Umma,
madaktari hao watasimamishwa kazi na kurudishwa kwa mwajiri wao ambaye
ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii,"alisema.


Aidha, alisema kuwa kwa ujumala madaktari hao waligomea barua zote
mbili yaani ya kuitwa kwenye kikao pamoja na ile ya kuwataka kujieleza
hivyo Bodi imechukua hatua za kisheria za kuwafukuza kazi.


Hata hivyo Mwenyekiti huyo wa bodi, alisema kuwa tayari hospitali ya
Rufaa kwa ushirikiano wa Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya, madaktari watano
wamepatikana ili kusaidia huduma kwa hospitali hiyo.

Chanzo: Mbeya Yetu

Wednesday, June 27, 2012

Dk. Mwakyembe afanya ziara ya kushitukiza Msamvu

Best Blogger Tips
 WAZIRI wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, amefanya ziara ya kushitukiza katika Kituo cha Mabasi cha Msamvu, Manispaa ya Morogoro na kufanya ukaguzi wa mabasi ya abiria yaendayo mikoani.

Katika ukaguzi huo, mabasi matatu aliyaamrisha yalipe faini ya Sh 250,000 kila moja, kutokana na makosa mbalimbali, likiwamo la kutokuwa na dereva wa akiba.

Ziara hiyo aliifanya mapema wiki hii asubuhi, kwa kushirikiana na maofisa wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) na lengo lake ni kukagua mabasi yanayofanya safari za mikoani na nje ya nchi na kuona kama yanakidhi vigezo katika shughuli ya kusafirisha abiria.

Katika ziara hiyo, Dk. Mwakyembe, alifika katika kituo hicho cha mabasi na kuegesha gari lake mbali kidogo, kisha kuelekea katika mabasi huku akiwa kama abiria na kuingia ndani ya mabasi hayo kisha kuanza kukagua leseni za madereva na vitambulisho vya kampuni za mabasi wanavyotumia madereva.

Ukaguzi mwingine alioufanya ni ratiba za safari pamoja na usalama wa mabasi na baadaye aliamrisha madereva walioonekana kuwa na makosa kulipa faini.

Mabasi yaliyolipishwa faini ni pamoja na Royal Coach linalofanya safari zake kutoka Dar es Salaam kuelekea Bukoba, ambalo dereva wake hakuwa na kitambulisho cha kampuni, basi la Super Najimunisa na Muro Investment yanayofanya safari zake Dar es Salaam kuelekea Mwanza ambayo yalikuwa na kosa la kutokuwa na dereva wa akiba.

Baada ya kubaini makosa hayo, aliwataka madereva ambao walionekana kuwa na makosa kulipa faini ya papo hapo, vinginevyo aliwataka SUMATRA kuwafikisha mahakamani, hata hivyo, madereva hao walikubali kulipa faini hiyo baada ya kuwasiliana na wamiliki wa mabasi wanayofanyia kazi.

Akizungumza na maofisa wa SUMATRA na madereva, alisema makosa kama hayo yanaweza kusababisha ajali za barabara na hivyo kupoteza maisha ya watu, vilema vya kudumu na uharibifu wa mali na ataendelea kufanya ziara za namna hiyo mara kwa mara kwa ajili ya kubaini makosa mengine.

Aidha, aliwataka SUMATRA na kikosi cha usalama barabarani kusimamia sheria za usalama barabarani na kutowaonea aibu madereva watakaoonekana kuwa na makosa, kwa kuwa kufanya hivyo kutasaidia kupunguza ajali ambazo ni tishio hapa nchini.

Kwa upande wake, Mkuu wa Usalama Barabarani mkoani hapa, Leonard Gyindo, alisema Kikosi cha Usalama Barabarani kimejipanga kudhibiti ajali za barabarani kwa kufanya ukaguzi kabla ya gari halijaondoka katika kituo hicho na kwa madereva wenye makosa wamekuwa wakilipishwa faini ya papo hapo na wengine kufikishwa mahakamani.

Hata hivyo, alimpongeza Dk. Mwakyembe kwa jitihada zake katika kusimamia sheria, hasa za usalama barabarani na kuahidi kuwa kikosi hicho kitampa ushirikiano na kutekeleza maagizo yote atakayotoa.
Chanzo: Mtanzania

Lowassa, Zitto wamtega JK

Best Blogger Tips
 NAIBU Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Zitto Kabwe, ameitaka serikali ya Rais Jakaya Kikwete kuwachunguza na kuwachukulia hatua zikiwemo kuwataja, kuwashtaki na kuwafilisi mafisadi wanaodaiwa kupora fedha za miradi ya gesi, madini na petroli na kuzihifadhi kwenye akaunti nchini Uswisi.

Aliyasema hayo bungeni jana wakati akichangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na kuongeza kuwa kuna wizi wa fedha za serikali zaidi ya sh bilioni 300 ambazo baadhi ya watumishi wa serikali wamepewa kama hongo na wawekezaji wa sekta hiyo.

Wakati Zitto akisema hayo, Waziri Mkuu wa zamani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ulinzi, Mambo ya Nje na Usalama, Edward Lowassa, ameitaka serikali kutolea maelezo madai ya kufichwa kwa shilingi bilioni 300 katika benki mbali mbali nchini Uswisi ambazo zinadaiwa kuwekwa na wanasiasa na watu wa kada mbalimbali nchini.

Akizungumza Bungeni jana Zitto aliitaka Ofisi ya Waziri Mkuu, vyombo vya usalama na Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) kuchunguza na kuchukua hatua mara moja.

Zitto aliitaka serikali kuiga mfano wa India ambayo ilipata mkasa kama huo na kuwataja watuhumiwa, kuwachunguza na kuzirudisha serikalini pesa zilizoonekana kuwa zilipatikana kinyume cha sheria.

Alitaka serikali ihakikishe kuwa watuhumiwa hao wanatajwa, wanachukuliwa hatua na pesa zinarudishwa nchini huku akionya kuwa inashangaza hata kabla ya miradi kuanza watu wameanza ufisadi na kupora mali za umma.

Gazeti la The Guardian la Jumamosi iliyopita lilichapisha taarifa za ufisadi huo uliofanywa na Watanzania sita waliopokea hongo kutoka makampuni yanayotafiti gesi, madini na petroli na kuweka pesa zao Uswisi.

Kwa upande wake Lowassa alitoa kauli hiyo jana wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari waliotaka kujua msimamo wa kamati ya ulinzi na usalama juu ya kuwepo kwa fedha hizo katika mabenki hayo ya Uswisi huku Watanzania wakiendelea kutaabika kwa mfumko mkubwa wa bei.

Akizungumzia kuhusu hilo, Lowassa ambaye hakutaka kuzungumzia kwa kirefu alisema hata wao kama kamati wamesoma taarifa hizo kwenye magazeti na kwamba wenye majibu mazuri kuhusiana na suala hilo ni serikali.

Hoja ya Zitto
Aidha Zitto katika hoja yake hiyo pia akizungumzia mjadala wa mafuta na gesi alishauri suala hilo lisiwe la Muungano kila upande uachiwe jukumu la kutafuta na kuchimba nishati hizo.
“Kila upande wa Muungano ushughulikie gesi na mafuta yake hakuna sababu ya kuchelewesha suala hili,” alisema.

Akiunga mkono hatua hiyo mbunge wa Nkasi Kaskazini (CCM), Ally Kessy, aliitaka serikali kutoa maelezo ya hatua zilizochukuliwa dhidi ya Watanzania walioingia mikataba ya rada.

Alisema Waingereza waliwashtaki watuhumiwa wake na kurudisha fedha ya rada kwa Tanzania na kuhoji serikali nayo imefanya nini kwa watuhumiwa walioingia mikataba mibovu ya rada humu nchini?
Alitaka waliofilisi mashirika ya umma kama Shirika la Ndege –ATC, Reli na Bandari wakamatwe, washtakiwe, kufilisiwa na kunyongwa hata kama walifanya hivyo miaka 20 iliyopita.

Aliliambia Bunge kuwa hata kama walioua mashirika wamekufa pingu zipelekwe kwenye makaburi yao na kusisitiza kuwa dawa ya walioua mashiriki ya umma ni kuuawa.

Alipendekeza wauliwe kwani wamewaua Watanzania kwa kuwaibia stahili zao kama dawa zilizokuwa ziwatibu na kusababisha vifo vyao.

Aliongeza kuwa sheria za Tanzania ni mbaya kwani zinawalinda wezi na kuwatetea mafisadi na kuiponda serikali kuwa ina masikio lakini haisikii ina pua lakini hainusi.
Aliishangaa miradi ya usafiri jijini Dar es Salaam iliyotangazwa na Waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli ya kujenga vituo saba vya usafiri wa boti kutoka Bagamoyo hadi Feri na kusema huo ni ubadhirifu wa fedha za umma.

Aliitaka serikali kuwashughulikia watuhumiwa wanaodaiwa kuhifadhi fedha za rushwa ya gesi na petroli kwenye benki za Uswisi na yenyewe kukaa kimya.
Aliongeza kuwa Takukuru imeshindwa kazi na inashangaza kuona kuwa inawaambia wananchi wawaletee majina ya wala rushwa wakati wanawajua na watu wanaiba fedha za umma na kujenga maghorofa na kumiliki mali za wizi.

Alisema maofisa wa Takukuru wanawachuuza wananchi wanaowapa majina ya wala rushwa kwa kutoa taarifa kwa watuhumiwa waliotajwa kisha kuwaomba rushwa.
Alikataa kuunga mkono bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa maelezo kuwa inaifanya mikoa mingine kuwa peponi na mingine kuwa motoni.

Nacho Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kupitia taarifa yake kilirudia kutoa wito kwa Rais Kikwete kutumia mamlaka yake ya kikatiba kuagiza kukamatwa kwa watuhumiwa wote wa ufisadi wa rada ambao iliwataja kwa nyakati mbalimbali ikiwemo katika orodha ya mafisadi (list of shame) Septemba 15 2007 katika Uwanja wa Mwembeyanga.

Katika taarifa iliyotolewa kwenye vyombo vya habari na kusainiwa na Mkurugenzi wa Mambo ya Habari wa CHADEMA, John Mnyika, alisema kutokana na sheria za usiri za Uswisi, wanaitaka serikali inayoongozwa na CCM kuwasiliana na serikali ya nchi hiyo ili kuanza mchakato wa kuwezesha mahakama za nchi hiyo kutoa ruhusa kutolewa kwa taarifa zote kuhusu wenye akaunti hizo na makampuni yaliyoweka kiasi hicho cha fedha ili hatua zaidi ziweze kuchukuliwa kwa mujibu wa Sheria za Tanzania na Sheria za Kimataifa.

“CHADEMA inatambua kwamba kuachwa kwa mafisadi bila kuchukuliwa hatua kamili za kisheria na mali zao kufilisiwa kunafanya taifa kuendelea na ufisadi ikiwemo ule wa Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), Richmond na sasa tuhuma mpya za ufisadi kwamba kuna vigogo wenye kiasi cha bilioni 303 kwenye akaunti Uswisi ambazo zinadaiwa kuwekwa na makampuni ya madini, mafuta na gesi asili,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Aidha chama hicho kimekumbusha kuwa katika orodha yake ya mafisadi iliwataja pia kwa majina viongozi wa serikali ambao waliingia mikataba ya kifisadi ya madini na rasilimali nyingine za taifa kutolewa kwa taarifa hizo za benki za nje kutathibitisha ukweli na pia kubainisha watuhumiwa wengine zaidi.

Pamoja na hilo imeitaka serikali inayoongozwa na CCM kuzingatia mpango kati yake na serikali ya Uingereza kupanga matumizi ya fedha kiasi cha shilingi bilioni 72.3 za rada zilizorejeshwa baada ya kubainika zilizochotwa kifisadi na kampuni ya BAE Systems ya Uingereza.

Wakati huohuo, CHADEMA imeshangazwa na uamuzi wa serikali inayoongozwa na CCM kubadilisha mpango wa kujenga nyumba za walimu kinyume na mpango huo wakati huu ambapo serikali iko katika mgogoro na walimu kutokana na kutowatimizia madai yao ya msingi ikiwemo nyongeza ya mishahara, kulipa madeni na kupunguza kodi kwenye mishahara.

Chama hicho kimeitaka serikali kukumbuka kwamba mpango huo ulikuwa moja ya ushahidi muhimu uliotolewa mahakamani kumshawishi jaji kutoa uamuzi wa kuridhia makubaliano kati ya SFO na BAE kwamba fedha hizo zingetumika kununua vitabu 4.4 milioni kwa ajili ya wanafunzi, vitabu 192,000 Kwa ajili ya walimu kufundishia, madawati 200,000, kujenga nyumba 1,196 za walimu wa shule za msingi vijijini, kujenga vyoo 200,000 kwenye shule za msingi.

Kadhalika imeonyesha kuguswa na taarifa kwamba zabuni ya kuchapa vitabu hivyo imetolewa kwa kampuni ya Kiingereza ya Oxford University Press hali ambayo itafanya sehemu kubwa ya fedha hizo kurejea hukohuko Uingereza.
Chanzo: Tanzania Daima

Dr Ulimboka azungumza kilichompata

Best Blogger Tips
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari nchini Dk Stephen Ulimboka, amepigwa na kujeruhiwa vibaya na watu wasiofahamika.

Dkt Ulimboka anadaiwa kuvunjwa mbavu, miguu yote miwili, kung’olewa meno yote ya mbele na kuumizwa vibaya katika sehemu mbalimbali za mwili wake.

Tukio hilo la kikatili na kusikitisha limetokea usiku wa kuamkia leo jijini Dar es Salaam, na linadaiwa kufanywa na watu wa sio julikana ambapo kabla ya kufanya unyama huo walidaiwa kumteka na kumpiga kabla ya kumtelekeza katika eneo la msitu wa Pande Mabwepande.

DKT. ULIMBOKA ASIMULIA TUKIO
Akisumulia tukio hilo Dkt Ulimboka alisema kuwa  jana usiku alipigiwa simu na mtu aliyejitambulusha kwake kuwa anaitwa Hemed, aliyemwambia kuwa anahitaji kuongea naye, na ndipo walipopanga kuonana katika eneo la Leaders Kinondoni.

Dk Ulimboka aliyekuwa akiongea kwa tabu, aliendelea kusimulia kuwa wakati akiongea na mtu huyo anayekiri kuwa alikuwa akifahamiana naye kabla, alikuwa na wasiwasi kwani kila mara alikuwa akipokea simu na kuwasiliana na watu wengine ambao hawakuwapo eneo hilo.

Alisema baada ya muda alishangaa kuona wanaongezeka watu wengine watano wakiwa na silaha, kisha wakamwambia kuwa anahitajika kituo cha Polisi na kumvuta na kumuangusha barabarani kabla ya kumuingiza katika gari lenye rangi nyeusi na kuondoka naye.

Dkt Ulimboka alisema kuwa wakiwa njiani walimpiga, na kumfikisha katika msitu huo wa pande na kuendelea kumpiga paka alipoteza fahamu.

MADAKTARI NAO WALONGA
Akisimulia mkasa huo mmoja wa madaktari wenzie aliyefahamika kwa jina moja la Dkt Deo, alisema kuwa alipigiwa simu na mtu hasiyemfahamu na kumfahamisha tukio hilo.

Alisema alipofika katika kituo cha Polisi cha Bunju, alimkuta akiwa katika hali mbaya na ilikuwa ngumu kumtambua kwakuwa alikuwa na majeraha mengi eneo la usoni.

Aliongeza kuwa akiwa na wenzie waliamua kumchukua na kumkimbiza katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kwaajili ya matibabu.

"Hali yake kwakweli ni mbaya sana, amepigwa mno na ameumizwa kwakweli tumemleta hapa hili aweze kupata matibabu, lakini mimi nilivyomkuta mara ya kwanza nilishindwa hata kumtambua kwa jinsi alivyokuwa ameumizwa"alisema Dkt Deo

Alisema kuwa alisimuliwa na Dkt Ulimboka kwamba watu hao waliomteka na kumpiga walikuwa na silaha na kwamba alishindwa kuwatambua.

Aliongeza kuwa Dkt Ulimboka alidai kuwa wakati akiwa katika halimbaya alikuwa akisikia mazungumzo yao, wakibishana juu ya kumuua wengine wakisisitiza achomwe sindano, na wengine wakitaka kumpiga risasi.

Alisema wakati mabishano yakiendelea kati yao, Dkt Ulimboka aliinuka akiwa na lengo la kukimbia lakini watu hao walipiga risasi hewani iliyomshtua na kuangua chini.

Kwa upande wake Dkt Cathbeth Mcharo ambaye ndiye aliyempokea Dkt Ulimboka Hospitalini hapo, alisema kuwa hali yake ni mbaya na kwamba wanajitahidi kumpatia huduma za haraka.

Alisema kuwa kwa hatua za awali amefanyiwa vipimo mbalimbali, hili iweze kufahamika aina ya matibabu anayotakiwa kupatiwa.

POLISI
Kamanda wa polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam Kamanda Suleiman Kova amezungumza na waandishi wa habari kuhusu tukio hilo la utekaji nyara na kujeruhi lililompata kiongozi mgomo wa Madaktari Steven Ulimboka anayedaiwa kutekwa na watu watano wakati akipata kinwaji katika klabu ya Leaders Kiondoni jijini Dar es salaam.

Kamanda Kova amesema Ulimboka aliokotwa na msamaria mwema ambaye hakutaka kumtaja jina lake kiusalama na kutoharibu upelelezi kuwa msamaria mwema huyo alimuokota Ulimboka katika msitu wa Mabwepande na kutoa taarifa kituo cha polisi cha Bunju, ambapo polisi aliyekuwa zamu alichukua maelezo yake na baadae Steven Ulimboka kuletwa katika hospitali ya taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi.

Kamanda Kova amesema jeshi la Polisi Kanda Maalum limeunda jopo maalum kwa ajili ya uchunguzi na upelelezi wa tukio hilo la utekaji nyara, kwani ni tukio la kwanza kutoke nchini, ameongeza kwamba wahusika wote watakaobainika kuhusika na tukio hilo wachukuliwa hatua za kisheria na sheria itafuata mkondo wake ili kukomesha matukio mengine kama hayo

MUHIMBILI
Wakati hayo yakitokea inadaiwa kuwa Askari Kanzu mmoja alikumbana na kipigo kikali kutoka kwa madaktari hapo Muhimbili kwa kile kilochodaiwa kutambuliwa na Dkt Ulimboka kuwa mmoja wa watu walio mjeruhi.

Pia inadaiwa kuwa Askari huyo aliingia chooni na kufanya mawasiliano na wenzake huku Madaktari hao wakimsikiliza na kutokana na alichokua akiongea chooni humo ndipo alipotoka aliambulia kichapo kikali.

Pia baadhi ya madkatari na wauguzi walikuwa wakisukuma gari alilokuwa amepanda Dkt Ulimboka huku wakiimba nyimbo za Umoja na Mshikamano Daima miongoni mwao.

Hali ya ulinzi ilikuwa kali Hospitalini hapo kwani Picha zilikuwa haziruhusiwi kupigwa.
Chanzo: Father Kidevu

Sunday, June 24, 2012

Musri wa Muslim Brotherhood mshindi

Best Blogger Tips
 Mohammed Mursi ametangazwa mshindi katika uchaguzi wa Rais nchini Misri.

Mursi ameshinda kura kwa asili mia 51.7% akimshinda mpinzani wake wa karibu Ahmed Shafik kwa mujibu wa tangazo la tume ya uchaguzi wa juu wa Rais.

Mkuu wa jopo la Majaji, Farouq Sultan, amesema kua wamezingatia malalamiko 466 kutoka kwa wagombea, ingawa matokeo ya uchaguzi hayatobalika.

Tangazo hilo lilifuatiwa na shangwe na vigelegele katikakati ya medani ya Tahrir mjini Cairo ambako wafuasi wengi wa Bw.Mursi walikua wamekuanyika.

Wafuasi hao wamekaa kwenye medani hio kwa siku kadhaa wakionyesha msimamo wao wa kuchukia sheria kadhaa zilizotangazwa na Baraza la juu la utawala wa majeshi ambayo wanadai zimeundwa ili kupunguza mamlaka ya Rais na kuelekeza uwezo mkubwa kwa majeshi.

Wafuasi wa Bw.Shafiq nao waliweka kambi yao katika eneo la kaskazini mwa mji ambako kuna makao makuu ya Tume ya uchaguzi huko Nasser City.

Akitangaza matokeo ya uchaguzi Jaji Sultan alianza kwa kunena kua tangazo la matokeo ya uchaguzi yalikua yamezongwa na shinikizo pamoja na hali ya wasiwasi.

Tume ya uchaguzi ilizingatia sheria ilipochunguza visanduku vya kupigia kura, na Jaji.Sultan alisema hakuna kilicho juu ya sheria.

Jaji huyo akaongezea kukanusha madai mawili nyeti kuhusu njama za kuibia uchaguzi, kwamba baadhi ya karatasi za kupigia kura ziliwekwa ndani ya visanduku tayari zikiwa na majina ya mgombea wanayemtaka ashinde.

Hatimaye Jaji Sultan akamtangaza mshindi kua ni Bw.Mursi ambaye ni Mwenyekiti wa chama cha Muslim Brotherhood cha Freedom and Justice, Bw.Mursi.

Baada ya dakika kadhaa akitangaza marekebisho kuhusu matokeo madomadogo ya kura ndipo akamtangaza Bw.Mursi kua mshindi kwa kuzoa kura 13,230,131, na Bw.Shafiq akiweza kuzoa 12,347,380, sawa na asili mia 48.27%.
Chanzo: BBC

Friday, June 22, 2012

Mahakama Kuu Yapiga Stop Mgomo wa Madaktari

Best Blogger Tips

Kufuatia Tangazo la Chama cha Madaktari nchini (MAT) la kuanza mgomo siku ya Jumamosi tarehe 23 Juni, 2012, Mahakama Kuu ya Tanzania,Kitengo cha kazi,Dar es Salaam imetoa amri ya kusitisha mgomo huo mpaka hapo pande zote mbili yaani Serikali na Chama cha Madaktari Tanzania (MAT) yatakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.

·Amri hiyo ya Mahakama imetolewa kufuatia maombi namba 73 ya 2012 yaliyowasilishwa chini ya hati ya dharura na Mwanasheria Mkuu wa Serikali dhidi ya Chama cha Madaktari Tanzania (MAT).Sababu za msingi amabazo zimepelekea Mahakama kuu kutoa amri hiyo upande mmoja ni pamoja na;·  
     
 *Iwapo mgomo huo utatokea utakuwa na kuwa amri hii isipotolewa madhara yake ni makubwa isiyoweza kufidiwa kwa namna yoyote ile kama vile kupoteza maisha n.k

· *Wajibu maombi, ambao ni MAT, inaundwa na Madaktari ambao wapo katika Sekta ambayo inatoa huduma mahsusi (essential service sector), Aidha Chama cha Madaktari Tanzania kimetangaza mgomo bila kufuatia taratibu zilizoanishwa katika Kifungu cha 76(1 na 2) cha Sheria ya Kazi (Employment and Labour Relations Act No 6 ya 2004.Masharti hayo ni ·    *Kuzuia wafanyakazi walio katika Sekta Muhimu kugoma na kama wakigoma, ·   *Kuwepo na makubalianao ya pamoja ya kutoa huduma za msingi wakati mgomo ukiendelea.

Kwa misingi hii, Mahakama Kuu ya Tanzania, kwa Chama cha Madaktari Nchini, na wanachama wake, inaamuru kusitisha na kutoshiriki katika mgonmo huo.

Thursday, June 21, 2012

Akatwa kiganja kwa tuhuma za kutembea na mke wa mtu

Best Blogger Tips
MWANAFUNZI wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari ya Nyakamwaga wilayani Geita, Fikiri Mtasimwa, amenusurika kifo baada ya kujeruhiwa kwa mapanga sehemu mbalimbali za mwili wake na kukatwa kiganja cha mkono wake wa kushoto na Baba Neema baada ya kumtuhumu kutembea na mke wake.
Akizungumza mjini hapa jana katika wodi aliyolazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Geita, mwanafunzi huyo ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Gengetano, Kata ya Nyakamwaga, alisema alikutwa na mkasa huo Juni 17, mwaka huu, usiku wakati akinywa uji kijijini hapo.

Alisema mwanamume huyo alimvamia katika kijiwe hicho cha uji na kuanza kumshambulia kwa mapanga sehemu za kichwani, mgongoni na begani, kabla ya kumkata mapanga katika mkono wake wa kushoto na kupelekea kiganja cha mkono wake huo kunyofoka, akimtuhumu kutembea na mkewe, Mama Neema na kumuachia maumivu makali.

“Wakati nakunywa uji kwenye kijiwe hicho mara alitokea huyo jamaa na kumuuliza muuzaji wa uji (Mektirida) kama kuna huduma hiyo, alijibiwa vizuri kwamba uji upo na ndipo baadaye nilimuona anachomoa panga kiunoni mwake na kuanza kunikata kwa kunilenga shingoni.

“Nilikwepa lakini bahati mbaya lilitua kisogoni na kunijeruhi na ndipo nilipoamua kukimbia, lakini sikufika mbali kwani nilidondoka chini, akanifuata na kunikata panga jingine la pili kichwani, sikukata tamaa nilinyanyuka tena na kukimbia huku damu zikiendelea kuvuja, nikadondoka tena kwa mara nyingine akakata jingine la tatu nikajikongoja na kunyanyuka nikakimbia huku nikikinga shingo asinichinje.

“Lakini kwa kuwa jamaa alivyoonekana alikuwa na lengo la kuniuwa hakukata tamaa alizidi kunikimbiza na baada ya kuanguka chini kwa mara nyingine tena alinifuata nilipokuwa nimeangukia na kuanza kukata mkono wangu wa kushoto.

“Alikata panga la kwanza, la pili, la tatu na la nne lilipelekea kiganja kunyofoka na ndipo rafiki yangu mmoja aitwaye Fikiri William, ninayesoma naye kidato cha tatu alipofika kunisaidia na ndipo mwanamume huyo alipoogopa kukamatwa na kuamua kukimbia kusikojulikana,” alisema Mtasimwa.

Alisema kutokana na majeraha hayo alipoteza fahamu na alizinduka akiwa wodini na hakumbuki ni akina nani waliompa msaada wa kumwahisha hospitalini.

Alisema siku moja kabla ya tukio hilo alikutana na mwanamume huyo njiani na kwa kuwa alikuwa akimheshimu kama kaka yake, alimsalimia lakini aligoma kuitikia salamu yake zaidi ya kumpa vitisho.

“Nakumbuka siku moja kabla ya tukio nilikutana naye nilipomsalimia alinijibu wewe kijana unadharau sana wala sihitaji salamu yako, ila kaa ukijua maisha yako ni mafupi sana na utakufa kifo kibaya,” alisema Mtasemwa.

Alisema kutokana na majibu ya mtuhumiwa alipojaribu kuhoji kulikoni ajibiwe hivyo, alidai hakupata ufafanuzi wowote na mwanamume huyo aliondoka akimuacha na maswali mengi kichwani mwake yasiyokuwa na majibu na siku ya tukio ndipo alijua maneno aliyomwambia siku moja kabla hayakuwa ni utani.

Alisema kutokana na hali duni ya kipato cha wazazi wake anajishughulisha pia na upigaji picha, kwa ajili ya kupata mahitaji muhimu ya shule na familia yake na kati ya wateja wake wakubwa mke wa mtuhumiwa naye alikuwa miongoni mwa watu hao na anadhani inaweza kuwa sababu ya kuhisiwa kutokana na kumpiga picha mwanamke huyo.

“Unajua sisi ni masikini wa kipato na ninaishi na mama baada ya kutengana na baba na ninajishughulisha na kupiga picha mtaani baada ya muda wa masomo na mke wa jamaa aliyenifanyiwa unyama huo alikuwa ni mteja wangu, naona ndiyo sababu mwanaume huyo alihisi natembea naye japokuwa sina tabia hiyo na nilikuwa namheshimu kama dada yangu,” alisema Mtasimwa.

Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali hiyo, Dk. Ndallo Ndallo, alithibitisha kuwapo kwa majeruhi huyo katika hospitali hiyo, aliyelazwa wodi namba nane na kuongeza kuwa hali yake ni mbaya kutokana na majeraha aliyoyapata sehemu mbalimbali za mwili wake na juhudi za kuokoa maisha ya mwanafunzi huyo zinaendelea.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Leonard Paulo, alithibitisha kuwapo kwa tukio hilo na juhudi za kumsaka mtuhumiwa huyo zinaendelea baada ya kutoroka na kukimbilia kusikojulikana.

Alisema mke wa mtuhumiwa pia alitoroka baada ya kupatiwa taarifa na majirani zake kuwa mumewe huyo amepanga kumchinja baada ya kutoka kumjeruhi kijana huyo.
Chanzo: Mtanzania

Wednesday, June 20, 2012

Mbunge CCM ajilipua

Best Blogger Tips
 KATIKA kile kinachoweza kutafsiriwa kama ujasiri wa kujitoa kafara, Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM), ameungana na wabunge wa kambi ya upinzani kuipinga bajeti ya serilaki ya mwaka 2012/2013 iliyowasilishwa bungeni Alhamisi ya wiki iliyopita.

Tofauti na wabunge wengine wa chama hicho tawala, wanaochangia mjadala wa bajeti hiyo kwa kutumia muda mwingi kuisifu bajeti hiyo na kuporomosha kejeli kwa ile ya wapinzani, Mpina kama alivyokuwa ametahadharisha hapo awali, jana hakuuma maneno.

Akichangia mjadala huo kwa kujiamini, aliwataka wabunge wenzake kumsaidia Rais Jakaya Kikwete, kuiondoa bajeti hiyo bungeni ili iweze kufanyiwa marekebisho katika maeneo mbalimbali ambayo hayako sawa.

Alisema kuwa hakubaliani na bajeti hiyo kwa sababu fedha zilizotengwa kwenye bajeti iliyopitishwa na Bunge mwaka jana hazikupelekwa zilikokusudiwa, na hivyo kusisitiza kwamba hatakuwa tayari kuiunga mkono, hadi hapo serikali itakapoleta maelezo kuhusiana na fedha hizo ili Bunge lijiridhishe kama hazikwenda kwenye maeneo waliyoyaidhinisha ijulikane zimekwenda wapi na kwa idhini ya nani.

“Matumizi yanayozungumzwa hapa, asilimia 87 hayahusiani na matumizi yalivyo katika fedha zinazopelekwa katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya matumizi ya miradi,” alisema.

Mbunge huyo ambaye alikuwa akishangiliwa na wabunge wa upinzani, huku wenzake wa CCM wakimwangalia kwa utulivu na wengine wakinong’ona, alidai sababu nyingine inayomfanya akatae bajeti hiyo, ni kitendo cha Bunge kuanza kujadili bajeti mpya wakati hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mwaka wa 209/2010 hazijajibiwa.

Alisema kwa kufanya hivyo serikali imevunja sheria ya nchi kifungu cha 40 ya kulitendea haki Bunge hilo kwani zilipaswa kujadiliwa kabla ya kuleta bajeti mpya ili Bunge hilo lijiridhishe.

Aidha, alisema serikali imevunja sheria ya ukaguzi ya mwaka 2008 kifungu cha 40 1-3 ya kulitendea haki Bunge hilo ili lijadili na kujiridhisha kama matumizi ya fedha za Watanzania zimefanya kazi iliyokusudiwa.
Mpina aliongeza kuwa, Bunge linatakiwa lijiridhishe na kuona kama kuna malalamiko ili liweze kuyajibu kabla ya kupeleka fedha nyingine.

“Si halali hata kidogo Bunge kuanza kujadili bajeti mpya wakati haya yote hayajatekelezwa, kwani kwa kufanya hivyo serikali imevunja sheria hiyo, na ilipaswa kupelekwa mahakamani kwani sheria ziko wazi kwa watu wanaovunja sheria,” alisema.

Akizungumzia matarajio ya Watanzania, Mpina alisema bajeti iliyowasilishwa si sahihi kwa kuwa imekiuka mpango wa maendeleo wa miaka mitano uliopitishwa na Bunge Juni 2011.

Mpina pia alisema bajeti hiyo imekinzana na azimio la Bunge na makubaliano ya kutenga sh trilioni 2.7 katika bajeti kila mwaka wa fedha ili zipelekwe katika miradi ya maendeleo, na asilimia 35 ya fedha za ndani zinazotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo zisitumike kwa matumizi mengine yoyote.

Alisema kwa kufanya hivyo, serikali imekiuka azimio la Bunge kwa sababu haikuzingatia hayo yote, ambapo badala ya kutenga sh trilioni 2.7 katika miradi ya maendeleo, imetenga sh trilioni 2.2 sawa na asilimia 30.

Mpina alisema wakati mapato yakiongezeka, matumizi yamepanda huku miradi ya maendeleo ikipunguziwa fedha kwani matumizi ya kawaida yamepangiwa sh trilioni 3.6.

Alisema wakati Watanzania wakisubiri ongezeko la utoaji wa huduma, serikali imekuwa ikienda kinyume na matarajio yao.

Alilitaka Bunge kumsaidia rais ikiwa amekosa watu wa kumsaidia na kuikataa bajeti ya sasa, kwa kuwa haina tija kwa wananchi.

Alisema kutokana na utekelezaji dhaifu wa mipango ya maendeleo, imewafanya Watanzania wengi kuondoa imani na serikali yao.

Mwishoni mwa wiki iliyopita, Mpina alisema ameamua kusimama katika ukweli na kuachana na ushabiki wa vyama, kwa manufaa ya Watanzania, akidai kuwa yuko tayari kuchukiwa na chama chake.

Spika awasuta wabunge
Katika hatua nyingine, Spika wa Bunge, Anne Makinda amewacharukia wabunge na kuwataka kujadili bajeti badala ya kuendeleza malumbano, kutoleana lugha za matusi na kuoneshana ufundi wa siasa bungeni.
Alisema kuwa hatua hiyo inawafanya wabunge kujiharibia wenyewe kwani wapiga kura wao wamekuwa wakiwaangalia muda wote na kumpigia simu, wakieleza kushangazwa na vitendo hivyo vya aibu wanavyovifanya.

Makinda alilazimika kutoa angalizo hilo kutokana na hatua ya wabunge kuendeleza malumbano ya vyama badala ya kujikita kwenye mjadala husika.

“Wabunge rudisheni heshima ya Bunge hili, kwani imepotea kabisa… acheni malumbano, jadilini mambo ya msingi ambayo yatasaidia kuboresha bajeti ili iweze kuwasaidia wananchi,” alisisitiza Spika Makinda.

Juzi, Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, alimtoa nje ya ukumbi wa Bunge mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), kwa madai kuwa alikiuka kanuni za Bunge kwa kutoa lugha isiyo ya staha, uamuzi uliopingwa na wapinzani wakisema wabunge wa CCM wanatukana pasipo kuchukuliwa hatua.

Makinda aliwataka wabunge kuheshimu kanuni, sheria na taratibu za Bunge hilo na kuacha kutumia lugha chafu na za matusi ili kurejesha heshima kama ilivyokuwa zamani.

“Mnatakiwa kutambua kuwa kila mbunge anayesimama hapa, wananchi wake wanamwangalia, hivyo mna kila sababu ya kujikita katika kujadili bajeti na si vinginevyo,” alisema.
Chanzo: Tanzania Daima

Matokeo ya uchaguzi Misri

Best Blogger Tips
 Tangazo la matokeo ya uchaguzi wa urais uliofanyika mwishoni mwa wiki limehairishwa, hii ni kulingana na taarifa kwenye televisheni ya kitaifa.

Matokeo hayo yalikuwa yatangazwe alhamisi, lakini tume ya uchaguzi imelazimika kuhairisha tangazo hilo ili kushughulikia malalamiko yaliowasilishwa na wagombea.

Wagombea hao Mohammed Mursi na Ahmed Shafiq wote wamedai kushinda uchaguzi huo.

Kulingana na tume ya uchaguzi jumla ya malalamiko 400 yamewasilishwa lakini haijasema matokeo hayo yatatangazwa lini.

Msemaji wa vuguvugu la Muslim Brotherhood, Nader Omran amesema kuwa tangazo hilo halifai kuhairishwa.

"Hatua hii itachochea hali ya wasiwasi itakuwa bora zaidi suala hili limalizwe alhamisi" amesema Bw Omran.
Wasimamizi wa kampeni ya mgombea wa Muslim Brotherhood, Mohammed Mursi wanasema kuwa kura zinaonyesha kuwa alishinda duru hiyo ya pili ya uchaguzi.

Lakini mshauri wa karibu wa Ahmed Shafiq, amewaelezea waandishi wa habari mjini Cairo kuwa, Shafiq- aliyekuwa waziri mkuu chini ya Utawala wa rais Hosni Mubarak-alishinda uchaguzi huo.

Maelfu ya watu wamekusanyika katika bustani ya Tahriri tangu juzi kulaani baraza kuu la jeshi ambalo juzi limejilimbikizia mamlaka baada ya mahakama kuu kulivunja bunge la nchi hiyo.
Chanzo: BBC

Tuesday, June 19, 2012

Msigwa amjibu Mwigulu

Best Blogger Tips
 Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji  Peter Msigwa amejibu pendekezo la Mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba la kutaka wapinzani waombewe, akisema hakuna kanuni yoyote ya uchumi inayosema Serikali ikiendesha mambo isivyo yanafanyika maombi.

Badala yake, alisema yeye ambaye ni mchungaji huwa wanaombea wazinzi na watu waotembea na wake za watu, na si matatizo ya kiuchumi.

“Inashangaza sana kuona watu wanaunga mkono bajeti…, kila mwaka deni la taifa linaongezeka na sasa limefika Sh20 trilioni, fedha ambazo ukizigawanya kila Mtanzania atakuwa anadaiwa Sh400,000” alisema Msigwa.

 “Nilivyokuwa naona wabunge wamevaa suti na wanachangia hoja bungeni nilipenda jambo hilo na kutamani siku moja niwe mbunge, lakini baada ya kuingia bungeni nimegundua kuwa hakuna kitu.”

Alisema bunge hilo hivi sasa halieleweki na kwamba mbunge mwenye elimu ya kutosha akisimama kuchangia hoja huwezi kumtofautisha na mtoto wa darasa la pili.

“Yaani mbunge profesa akisimama kuchangia hoja huwezi kumtofautisha na mtoto wa darasa la pili, watu wenye akili, akili zao wameziweka mfukoni na kuweka ushabiki wa vyama mbele, tumekuja bungeni kumaliza matatizo sio kuongeza matatizo” alisema Msigwa.

Huku akitumia mifano ya wanasaikolojia mbalimbali Msigwa alisema ni aibu kuona Watanzania wanazidi kuwa maskini harafu kila mwaka yanayozungumzwa ni tofauti na yanayotendeka.

“Ufikie wakati wabunge tutambue kuwa tumekuja hapa bungeni kuwatumikia wananchi, Watanzania waliotuchagua wanateseka na wabunge hapa bungeni mnazungumza maneno ya khanga tu,” alisema Msigwa.
Chanzo: Mwananchi

Mubarak yupo 'hali taabani'

Best Blogger Tips
 Taarifa za kutatanisha zimeibuka kuhusu afya ya Hosni Mubarak aliyeondolewa madarakani kufuatia maandamano ya kutaka mageuzi nchini Misri mwaka jana.

Baadhi ya vyombo vya habari vimetangaza kuwa uhai wake unasitiriwa kwa kutumia mashine baada ya kuhamishwa kutoka gerezani hadi kwenye hospitali ya kijeshi mjini Cairo.

Mubarak mwenye umri wa miaka 84 aliugua kiharusi akiwa jela, hali iliosababisha ahamishwe hadi hospitalini akiwa mahututi.

Kiongozi huyo aliondolewa mamlakani mwaka jana kufuatia maandamano ya raia wa nchi hiyo yakupinga utawala wake.

Mwezi uliopita alihukumiwa kifungo cha maisha jela kwa kosa la kuamrisha mauaji ya baadhi ya waandamanaji hao.

Mara kadhaa kumekuwepo na taarifa za kutatanisha kuhusu afya ya rais huyo wa zamani lakini kila mara zimepuuzwa.

Taarifa hizo kuhusu afya yake zimetokea wakati ambapo maelfu ya waandamanaji wamekusanyika kwenye bustani ya Tahrir kulaani uamuzi wa baraza la kijeshi wa kujilimbikizia mamlaka.

Maandamano hayo yamepangwa na viongozi wa vuguvugu la Muslim Brotherhood. Mgombea wa kundi hilo wa kiti cha urais Mohammed Musri anadai kushinda uchaguzi huo uliofanyika mwishoni mwa wiki.

Lakini pia mpinzani wake ambaye pia alikuwa waziri mkuu chini ya utawala wa Rais Mubarak, Ahmed Shafiq naye anadai ushindi.

Matokeo rasmi ya uchaguzi huo yatatanzagwa alhamisi.

Vuguvugu la Muslim Brotherhood limeahidi kumfungulia mashtaka mapya Hosni Mubarak punde tu litakapo pata madaraka na linataka ahukumiwe kifo.
Chanzo: BBC

Monday, June 18, 2012

Mkuu wa shule atandikwa viboko

Best Blogger Tips
 MKUU wa Shule Msaidizi katika Sekondari ya Ndedo wilayani Kiteto mkoani Manyara, amejeruhiwa vibaya baada ya kupigwa marungu na kuchapwa mwilini mwake na vijana wa jamii ya kifugaji wa Kimasai maarufu Morani.

Akizungumza juzi na waandishi wa habari nyumbani kwake baada ya kutoka hospitali ya Wilaya ya Kiteto, Mwalimu huyo, Hassan Didii alidai alipigwa na vijana hao wiki iliyopita baada ya kutoa adhabu ya kumchapa viboko mwanafunzi mmoja wa kidato cha pili wa shule hiyo.

Alidai kuwa morani hao walimchapa viboko na kumpiga rungu usoni, mgongoni na mikononi na kumuachia maumivu mwilini mwake baada ya mwanafunzi huyo kwenda kushtaki nyumbani kwao kuwa alichapwa.

Mwalimu Didii alidai hadi hivi sasa hali yake si nzuri kwani anajisikia maumivu mwilini mwake kutokana na majeraha aliyoyapata baada ya kupigwa na kundi la vijana hao wa jamii ya Kimasai.

Pia alilalamikia kitendo cha vijana hao kutochukuliwa hatua yoyote japokuwa alishatoa taarifa kwenye Kituo cha Polisi cha Mjini Kibaya.

Mganga wa zamu wa Hospitali ya Wilaya ya Kiteto ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini kwa kuwa si msemaji, alithibitisha kumpokea Mwalimu Didii akiwa na majeraha ya kupigwa na walimpatia matibabu na kuongeza kuwa hivi sasa hali yake inaendelea vizuri.

Askari Polisi anayeshikilia jalada la kesi hiyo ambaye pia hakutaka kutajwa jina lake gazetini, alithibitisha kwamba Mwalimu Didii alishatoa taarifa kwenye kituo hicho na hivi sasa wanajipanga kwenda eneo la Ndedo kwa kuwa kuna umbali mrefu kutoka Kibaya hadi eneo hilo.

Adhabu hiyo inafanana na aliyowahi kuitoa Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Albert Mnali ambaye Februari mwaka 2009, aliacha maswali miongoni mwa walimu baada ya kufanya ziara ya kushitukiza katika shule tatu za msingi za kata ya Katerero na kuamuru walimu 16 kucharazwa viboko kwa kile alichodai ni utoro na uchelewaji wao.

Mnali baada ya kuagiza adhabu hiyo, alikiri kuisimamia ifanyike kwa kuwa walimu hao ni wazembe waliochangia wilaya yake kuibuka na matokeo mabaya katika mtihani wa darasa la saba mwaka jana.

“Nilimwita askari wangu nikamwambia Mwalimu Mkuu atoke, tukafunga mlango nikawaambia walimu kama watoto wanaochelewa mnawapa adhabu na mimi nawapa adhabu,” alisema Mnali kuthibitisha kucharazwa viboko vinne kila mmoja.

Alipoulizwa kama adhabu hiyo haikuwa udhalilishaji wa walimu, alikana na kusema haikutolewa mbele ya wanafunzi na kwamba yeye si mtu wa kwanza kutoa adhabu ya aina hiyo aliyoiita kuwa ndogo.

Mbali na kutoa ufafanuzi huo, alisema tayari amemwandikia Mkurugenzi juu ya adhabu hiyo akiambatanisha na majina ya walimu walioadhibiwa na kusema inabidi wachukuliwe hatua zaidi kwa vitendo vyao vya uzembe na utoro shuleni. Baada ya tukio hilo, Rais Jakaya Kikwete alimfukuza kazi Mnali kwa kitendo hicho.
 Source: Habarileo

Hotuba ya Bajeti ya Kambi ya Upinzani Bungeni

Best Blogger Tips
 I.          UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Kambi ya Upinzani, ninatoa maoni ya Kambi ya Upinzani kuhusu Bajeti ya Nchi ya mwaka wa fedha 2012/2013 kwa mujibu wa Kanuni za Bunge Kifungu cha 99(7) toleo la Mwaka 2007.

Mheshimiwa Spika, Natoa pongezi za dhati kabisa kwa Ndugu William Augustao Mgimwa, Mbunge wa Jimbo la Kalenga mkoani Iringa kwa kuteuliwa na Rais kuwa Waziri wa Fedha na Uchumi. Vile vile nawapongeza Ndugu Saada Mkuya na Ndugu Janeth Mbene kwa kuteuliwa kwao kuwa Wabunge na baadaye kuwa Manaibu Mawaziri katika Wizara hii nyeti sana.  Ninawapa pole pia maana Wizara ya Fedha sio Wizara lelemama. Kambi ya Upinzani itaendelea kuisimamia Wizara hii kwa ukaribu sana kama ilivyofanya katika kipindi cha miaka miwili iliyopita. Mtakapofanya vizuri tutawapongeza ili muongeze juhudi, mtakapoharibu tutawawajibisha.

Mheshimiwa Spika, Ni dhahiri kwamba Mwaka wa Fedha uliopita ulikuwa mwaka mgumu sana kwa Watanzania. Ni mwaka ambao gharama za maisha zilipanda kwa kasi kubwa sana na juhudi za Serikali kuwakwamua wananchi na hasa wananchi wanyonge kutoka kwenye lindi la ufukara ziligonga mwamba. Kambi ya Upinzani inawapa pole Watanzania kwani hili ndilo walilochagua. Muhimu ni kuvumilia mpaka uchaguzi ujao na kufanya mabadiliko ya Serikali ili kuweka Serikali itakayoongozwa na CHADEMA na itakayoweza kukabili changamoto za sasa na za baadaye.

Mheshimiwa Spika, naomba tufanye mapitio kidogo ya Bajeti inayomaliza muda wake.

  1. UTEKELEZAJI WA BAJETI ILIYOPITA
Mheshimiwa Spika, kabla ya kutoa bajeti mbadala ya Kambi ya Upinzani ni vema kufanya tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya Serikali iliyopita ili kuona ni kwa namna gani Serikali inathamini fedha za walipa kodi, na dhamira yake ya kuleta maendeleo ya kiuchumi katika Taifa. Katika kufanya hivyo, tutapitia baadhi ya maeneo ambayo Kambi ya Upinzani tunaona kuwa hayakutekelezwa katika bajeti iliyopita.

Kupunguza Makali ya Maisha

Mheshimiwa Spika, Katika Bajeti ya mwaka 2011/12 Serikali ilitangaza nia yake ya kupunguza makali ya maisha. Hatua mbali mbali zilichukuliwa ikiwamo kupunguza kodi na tozo kwenye mafuta ya Dizeli na Petroli, kuanza kutekeleza mpango wa dharura wa umeme na kutoa fedha za kununua chakula kwa Wakala wa Chakula. Serikali ilitumia shilingi bilioni 296 na dola za Marekani milioni 183 kwenye Umeme. Vilevile Serikali ilitumia shilingi bilioni 27 kununua Mahindi na kusambaza kwenye masoko.

Mheshimiwa Spika, licha ya hatua hizo zilizochukuliwa Mfumuko wa Bei uliongezeka maradufu kutoka wastani wa asilimia 6.3 mwaka 2010/11 mpaka wastani wa asilimia 17.8 mwaka 2011/12. Serikali imefeli katika lengo lake la kupunguza makali ya maisha kwa wananchi. Sio tu kwamba Serikali imeshindwa kudhibiti upandaji holela wa gharama za maisha bali pia hatua za Serikali zimeongeza kasi ya kupanda kwa makali ya maisha.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani Bungeni katika Hotuba yake mbadala ya mwaka 2011/12 iliitaka Serikali  kushughulikia msingi wa mfumuko wa Bei hapa nchini ambao ni uzalishaji mdogo wa mazao ya chakula. Tumeelezwa na Waziri Kivuli wa Mipango na Uchumi kwamba Chakula peke yake ni asilimia 48 ya kapu la bidhaa na huduma ambazo mwanachi anatumia. Mfumuko wa Bei ya Chakula kinacholiwa nyumbani na kwenye migahawa ilikuwa asilimia 25 mwezi Aprili 2012 (BoT monthly Economic Review, May 2012). Vile vile mfumuko wa bei wa nishati inayotumika nyumbani na mafuta ya Dizeli na Petroli ulifikia asilimia 25 pia mwezi Mei mwaka 2012. Ni dhahiri kwamba iwapo tutadhibiti mfumuko wa bei ya chakula tutaweza kushusha mfumuko wa bei kurudi kwenye tarakimu moja.

Mheshimiwa Spika, Serikali inapendekeza hatua zilezile ilizofanya mwaka wa fedha unaokwisha kwa kutoa vibali kwa Wafanyabiashara vya kuagiza Mchele na Sukari. Katika hotuba yake Waziri wa Fedha anasema ‘….Serikali ilitoa vibali vya kuagiza sukari bila kutoza ushuru wa forodha kiasi cha tani 200,000 ili kukabiliana na uhaba na kupanda kwa bei ya Sukari…’(uk 9 ibara ya 15). Baada ya hatua hii bei ya Sukari ilipanda kutoka tshs 1700 mpaka tshs 2800 kwenye maeneo mengi nchini. Waziri wa Fedha katika hotuba yake anatoa suluhisho. Ninanukuu. ‘…hatua za haraka ambazo Serikali itachukua ni pamoja na kutoa vibali vya uagizaji wa Sukari na mchele kutoka nje….’! Serikali inachukua hatua zilezile kwa tatizo lile lile ikitegemea matokeo tofauti.
Endelea kusoma hotuba hii......
Chanzo: Matukio - Michuzi

Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits