Monday, March 19, 2012

Dk Mwakyembe aweka hadharani ugonjwa wake

Best Blogger Tips
 BAADA ya utata wa muda mrefu wa ama Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk Harrison Mwakyembe amelishwa sumu au la, jana Mbunge huyo wa Kyela, aliweka hadharani ugonjwa wake akisema unafahamika kitaalamu kwa jina la Popular Scleroderma huku akisisitiza: “Sasa nimepona kabisa.”

Dk Mwakyembe amekuwa akisumbuliwa na maradhi ya ngozi ambayo mwaka jana yalizidi kumtikisa na Oktoba 9, Serikali iliamua kumpeleka Hospitali ya Appolo, India kwa ajili ya matibabu na uchunguzi zaidi.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam jana, Dk Mwakyembe akiwa amevalia kofia ya pama alisema: “Si kwamba sijambo, bali nimepona kabisa baada ya kugundulika na maradhi hayo na kutibiwa.”

“Nimerudi juzi kutoka India na daktari wangu ameniambia nimepona, nilikuwa nasumbuliwa na maradhi ya ‘Popular Scleroderma’ iliyosababisha ‘skin disorder’ (ngozi kutokuwa katika hali ya kawaida), lakini kwa nguvu za Mungu nimepona, namshukuru Mungu.”

Kuhusu sumu
Alipoulizwa kuhusu tuhuma za kulishwa sumu, Dk Mwakyembe alikataa kuzungumzia hilo akisema anasubiri uchunguzi ulioagizwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Shamsi Vuai Nahodha.

Hata hivyo, Dk Mwakyembe alisema angependa kuona uchunguzi huo unakamilika haraka na ripoti yake inatangazwa kwa umma.

Alisema yuko tayari na anasubiri tume hiyo ya uchunguzi iliyoundwa na Waziri Nahodha imhoji ili atoa kile kilichomo katika ripoti ya daktari wake.

Dk Mwakyembe alisema anachoshukuru hadi sasa ni kwamba afya yake imeimarika kutokana na shinikizo la Rais Jakaya Kikwete ambaye aliagiza Serikali kumpa kipaumbele wakati wote akiwa nchini na India hatua ambayo imemwezesha kufika hapo alipo.

Kutokana na hali hiyo, Dk Mwakyembe aliwataka wananchi wote wakiwemo wa jimboni kwake Kyela kuondoa wasiwasi akisema sasa yupo imara kwa ajili ya ujenzi wa majukumu ya taifa.

“Ninaomba wapiga kura wangu wa Kyela waache jazba, wawe na subira juu ya matatizo yangu. Wiki ijayo nitakwenda kuzungumza nao ili niweze kuwaeleza matatizo yaliyokuwa yananisumbua, lakini sasa hivi niko fit,” alisema.

Mtaalamu auzungumzia
Mtaalamu wa afya ambaye hakutaka kutajwa gazetini alisema ugonjwa huo wa ‘Popular Scleroderma’ unasababishwa na chembechembe hai nyeupe kushambulia kitu kigeni kilichoingia kwenye mwili na kusababisha magonjwa ya ngozi.

Alisema chembechembe hizo zinaweza kusababisha ngozi ya mwili kuharibika... “Ni magonjwa yanayosababishwa na chembechembe hai nyeupe kujikataa zenyewe na kusababisha ugonjwa wa ngozi na mifupa.”
Kauli hiyo ya Dk Mwakyembe kuhusu ugonjwa wake imefungua ukurasa mpya hasa baada ya baadhi ya wanasiasa kuamini kuwa hakuwa na tatizo jingine bali, amelishwa sumu. Tayari Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba ambaye alitoa ripoti akisema Naibu Waziri huyo hakulishwa sumu kama inavyodaiwa, amefanyia uchunguzi madai hayo na kukabidhi jalada lake kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma, DPP ili afungue kesi.

Kauli ya Sitta

Mmoja wa wanasiasa waliodai kuwa Dk Mwakyembe amelishwa sumu, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samwel Sitta alipoulizwa jana juu ya kauli hiyo mpya ya Dk Mwakyembe alisema hana cha kuzungumza.

Januari 28, mwaka huu akiwa kwenye uzinduzi wa Programu ya Neno la Hekima kutoka kwa Kiongozi iliyoanzishwa na Kanisa la Ufufuo na Uzima la Kawe, Dar es Salaam Sitta alisema Dk Mwakyembe amelishwa sumu.

Akizungumza kwa utaratibu, Sitta alisema hana mengi ya kuzungumza kuhusu ugonjwa unaomsumbua Dk Mwakyembe na kusisitiza kuwa isubiriwe ripoti kutoka India ambako alikuwa akitibiwa.

“Dk Mwakyembe si anatibiwa India?,” alihoji na kuendelea, “Nadhani umeshapata jibu, tusubiri… acha huko India waendelee na uchunguzi wao, siwezi kusema lolote zaidi ya hilo nililokuambia.”

Dk Mwakyembe alianza kuugua Oktoba 9, mwaka jana na alitibiwa Apollo hadi aliporejea Desemba 11, mwaka jana. Alirejea tena India kuendelea na matibabu hadi Ijumaa iliyopita aliporudi na kusema kuwa amepona.

Matatizo yake ya kiafya yamesababisha mvutano baina ya viongozi wa Serikali. Wakati Manumba akisema ripoti kutoka Wizara ya Afya ilionyesha hakupewa sumu, waziri mwenye dhamana na afya Dk Haji Mponda alimkana.

Pia Waziri Nahodha ambaye ana dhamana na jeshi hilo la polisi, alikana ripoti hiyo ya DCI Manumba na kutaka aulizwe mwenyewe alikoitoa huku akisema uchunguzi alioagiza bado unaendelea.

Ugonjwa wa Scleroderma

Kwa mujibu wa mtandao wa Johns Hopkins wa www.hopkinsscleroderma.org, Scleroderma ni ugonjwa unaohusisha mfumo wa kinga ambao wakati mwingine dalili zake zinaweza kuwa mtu kuwa na baridi yabisi na sugu. Ni ugonjwa unaoathiri mwili, hasa muunganiko wa tishu na kuufanya kuwa mgumu.

Mfumo wa Kinga
Scleroderma iko katika kundi la ugonjwa wa mfumo wa kinga. Hii ina maana kwamba mfumo wa kinga wa mtu hufanya kazi kwa kujitegemea. Hulinda mwili dhidi ya maadui mbalimbali kama virusi na maambukizi.

Kuwa na ugonjwa huo wa mfumo wa kinga maana yake ni tishu au kinga kuvamiwa na wageni, ama virusi au maambukizi mengine na hivyo kusababisha matatizo.Mtu anapokuwa na scleroderma, seli huathirika kwa sababu katika hali ya kawaida seli haipaswi kuwa na kitu kingine cha ziada katika mfumo wake wa utendaji kazi na kama ikitokea hivyo, mtu huyo hujikuta katika matatizo yanayosababisha mfumo wa mwili wake kutokuwa kama ulivyo kawaida.
Unawezaje kuupata?
Watu wachache hupata ugonjwa huu na hakuna anayejua unatokana na nini. Scleroderma ni ugonjwa nadra. Chini ya watu 500,000 Marekani wanasumbuliwa nao na hakuna anayejua kwa uhakika chanzo chake.
Baadhi ya wataalamu wanabainisha kuwa watu kati ya saba wenye kusumbuliwa na ugonjwa huo ni wanawake. Wenye kusumbuliwa zaidi na ugonjwa huo ni wale wenye umri wa kati ya miaka 35 na 50. Hata hivyo, watoto wadogo na watu wazima zaidi wanaweza kuupata.
Baadhi ya familia zimekuwa zikiathirika zaidi na ugonjwa huu kuliko zingine. Ingawa scleroderma hauonekani kuathiri kifamilia, lakini mara nyingi hutokea katika familia ambayo imewahi kuwa na mtu mwenye magonjwa yanayokaribiana nao kama vile tezi au mengine yanayofahamika kitaalamu kama arthritis rheumatoid au lupus ambayo msingi wake ni kuathirika kwa mfumo wa kinga.

Dalili za awali
Kwa baadhi ya watu kuna dalili mbili za kwanza:
• Vidole kuwa vya baridi na wakati mwingine kubadilika rangi au mtu kuonekana mwenye msongo wa mawazo.
• Vidole na mikono kuwa migumu na kutoa magamba au unga
Mabadiliko ya rangi ya kidole husababishwa na kupungua kwa uwezo wa mishipa ya damu kupitisha damu ipasavyo. Hii hutokea kwa sababu ya madhara yaliyotokea dhidi ya mishipa ya damu iliyoharibiwa kutokana na ugonjwa huo.
Hali ya ubaridi na mabadiliko ya rangi huitwa raynaud’s (hutamkwa ray-knowds). Watu wengi wenye hali hii wanaweza kudumu nayo bila kuwa na ugonjwa wa scleroderma.

Athari tofauti
Athari ya scleroderma inatofautiana sana kati ya watu. Wengi huanza kuona dalili za vidole kubana na hata kuvimba. Kisha kwa baadhi ya watu huchukua miezi sita wakati wengine hata zaidi ya mwaka ugonjwa kujitokeza rasmi.
Chanzo: Mwananchi

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits