Wednesday, June 13, 2012

Msiahidi, tendeni

Best Blogger Tips
 Rai ya Jenerali Ulimwengu

JUMAMOSI iliyopita chama-tawala, CCM, kilionyesha kuwa kumbe bado kinaweza kukusanya maelfu kwa maelfu ya wanachama na mashabiki wake na kikawaweka kwa muda wakisikiliza hotuba baada ya hotuba za serikali wakieleza walichokifanikisha na wanachotaraji kukifanikisha katika kipindi kifupi kijacho.

Mkutano huo wa Jangwani ulihudhuriwa na watu wengi mno, na wengi walionekana wakiwa wamevaa sare za chama hicho, ambazo nazo zilionekana kama mpya. Kwamba chama hicho kliweza kuwakusanya watu wengi kiasi hicho ni jambo muhimu kwa sababu kwa muda mrefu kilikuwa kikionekana kama vile kimepigwa sindano ya ganzi na kimeduwaa.

Najua kwamba watazamaji na wachambuzi wengi  wamekuwa wakisema kwamba umati huo ulikuwa mkubwa kiasi hicho kwa sababu tu wakuu wa chama mkoani Dar es Salaam walitumia fedha nyingi sana kukodi magari ya kuwasomba wanachama hao, na kwamba baadhi yao walilipwa ili wahudhurie kikao hicho cha maonyesho.

Hata kama hilo ni kweli, ni kweli pia kwamba watu walikwenda Jangwani kwa hiari yao, kwa sababu hatujapata taarifa za ye yote aliyetekwa nyara na kubebwa kupelekwa Jangwani.

Jambo jingine la kuliangalia kama ushindi wa chama-tawala ni kile kitendo cha mawaziri wa Serikali kuonyesha kuwajali wananchi kiasi cha kujihisi kwamba wanawajibika kutoa taarifa za utendaji wa idara zao moja kwa moja kwa wananchi, jambo ambalo huko tulikotoka halikuzoeleka. Sasa inaelekea mawaziri wataanza utaraibu wa “kuripoti” moja kwa moja kwa wananchi, ambao sasa wanatambua kwamba ndio matajiri wao.

Jambo la tatu ambalo limajitokeza ni kwamba chama-tawala sasa kimeamua kujibu mapigo ya chama kikuu cha upinzani kwa kuchukua kauli za wapinzani hao na kuzikosoa huku kikionyesha kwamba ndicho kilicho na uhalali wa kuendelea kuitawala nchi yetu.

Ingawawaje mapema wakuu wa chama-tawala walitaka watu waamini kwamba lengo la mkutano huo wa Jangwani halikuwa “kujibu mapigo” ya CHADEMA , lakini mwenye masikio haambiwi sikia. Mkutano ule ulikuwa wa kujibu mapigo kuanzia mwanzo hadi mwisho na wala haukuwa na lengo jingine lo lote.

Jambo la nne nililolichukua kutoka mkutano ule ni kwamba chama-tawala kimeanza kampeni kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu ujao. Tumezoea kuwasikia wakuu wa chama hicho wakiwakosoa wapinzani kwa kufanya kampeni zisizokuwa na mwisho, wakisema kwamba uchaguzi umekwisha na kwa hiyo hakuna haja ya kufanya kampeni. Inawezekana kwamba msimamo wa kutokufanya kampeni hadi mwaka 2015 umeonekana kuwa na gharama kubwa kwa chama hicho na ndiyo maana kikaamua kufanya kama wafanyavyo wakuu wa CHADEMA.

Sasa, angalau tunajua kwamba vyama vikuu vya kisiasa nchini, CCM na CHADEMA, vimeingia katika kampeni ya kudumu, na kwamba kampeni hizi zitatusaidia kujua zaidi kuhusu sera na mipango ya vyama hivi. Ni upuuzi kutaka chama cha siasa kisifanye kampeni eti kwa sababu uchaguzi umemalizika, kisubiri hadi uchaguzi ujao. Ni sawa na kujiambia timu ya mpira isifanye mazoezi na isisajili wachezaji wapya kwa sababu ligi haijaanza.

Nasema kwamba kilichojitokeza Jumamosi iliyopita ni ishara kwamba chama-tawala hakiko tayari kuendelea kubamizwa na wapinzani wanaokikosoa kila siku kwa lengo la kukifanya kionekani kama hakifai kutawala, lengo la kimkakati likiwa ni kukiondoa madarakani. Sasa chama-tawala kitajibu mapigo, na hiyo ndiyo raha ya siasa, mapigo na majibu ya mapigo, hoja na majibu dhidi ya hoja.

Nitakachokitarajia sasa ni kwamba katika kujibu mapigo, chama-tawala hakitajitengenezea matatizo mengine zaidi ya yale kilicho nayo, kwamba hakitajitia kitanzini chenyewe bila kujua. Ni rahisi kwa kundi la watu waliohamanika kujisemea maneno bila kuyapima na baadaye kujuta kwa nini waliyasema maneno hayo.

Kwa mfano, katika mkutano ule katika viwanja vya Jangwani, sura iliyojitokeza ilikuwa ni Serikali zaidi kuliko chama-tawala. Ni kweli mawaziri waliokuwa Jangwani ni wanachama wa chama-tawala, na wala hilo haliwezi kuwa na shaka. Pia alikuwapo Katibu wa Itikadi na Uenezi pamoja na mlezi wa Mkoa wa Dar es Salaam. Lakini Mwenyekiti alikuwa wapi, Katibu Mkuu alikuwa wapi na Makamu Mwenyekiti alikuwa wapi? Ujumbe mzito wa Halmashauri Kuu ulikuwa wapi kudhihirisha dhamira ya kweli ya chama hicho ya kufanya kazi ya kujibu mapigo ya wapinzani kwa njia ya kudumu?

Ninachoshuku ni kwamba hii ilikuwa ni hatua ya zima-moto, maandalizi ya dharura ya kujaribu kupunguza kasi ya upinzani kwa kupitia huko huko walikopitia na kufanya yale yale waliyofanya wapinzani.
Ni ishara kwamba mambo yamebadilika sana. Kuna wakati katika miongo miwili iliyopita ambapo tulishuhudia vyama vya upinzani vikijaribu kuiga kila kilichofanywa na chama-tawala; sasa ni kinyume chake kwa sababu ni chama-tawala kinachoanza kuiga yanayofanywa na wapinzani.

Ni rahisi kuwaambia mawaziri waende Jangwani waeleze ni nini Serikali yao imefanya na ni nini inakusudia kufanya, kuliko kuwapelekea wakuu wa siasa ndani ya chama kwenda kuelezea siasa ambazo hata wao hajui zimekaa vipi na zinaelekea wapi. Hii ndiyo maana ya kuwapeleka mawaziri badala ya viongozi wa chama kama viongozi wa chama.

Isitoshe, ahadi ni deni, na tayari chama-tawala kimekwisha kujivisha madeni mpaka kinatakiwa kiogope kutoa ahadi nyingine. Kumekuwa na tabia ya kutoa ahadi za uongo “mchana kweupe’ ili watu wavutike na wakichague chama hicho, bila kuangalia athari zake katika siku zijazo. Mwaka 2010 tulisikia ahadi nyingine nyingi mno, ambazo kama zingekuwa zinatekelezwa leo hii zingeweza kuwa zimefikia nusu ya utekelezaji. Utekelezaji u wapi?

Miaka minane iliyopita, kwa mfano, tulisikia ahadi za kutengeneza ajira kwa mamilioni; mwaka 2010 hatukusikia sana hadithi za ajira, ingawaje wapo waliojaribu kusema kwamba ajira zimetengenezwa ingawa si wengi walioamini hadithi hizo.

Ni muhimu kwa wanasiasa kutambua kwamba hali ya nchi na wananchi wake imebadilika sana. Leo hii tunao watu wengi, na hasa vijana, ambao wanafutailia kwa makini na kwa karibu mno kila kitu kinachosemwa na kufanywa na watawala wao, na wanaweka kumbukumbu. Si watu wa kusikiliza na kisha kusahau walichokisikia.

Kwa bahati mbaya tumejenga utamaduni unaotaka kutufanya tuamini kwamba siasa ni uongo, na kwamba ili ufanikiwe katika siasa huna budi kuwa mwongo, na hilo ndilo tunalolishuhudia leo hii. Wanasiasa wetu si wanasiasa wa kweli bali ni waongo ambao hata katika uongo wao hawaonyeshi umahiri wo wote.

Haiyumkiniki kuwaambia wananchi kwamba  Serikali yao inashughulikia mfumuko wa bei na hali ngumu ya maisha wakati kila mtu anaona kwamba hali inazidi kuwa mbaya zaidi kila uchao.

Hata kama unachowaambia ni kwamba Serikali imenduka kutoka usingizini na sasa imejenga mikakati na mbinu kulishughulikia suala hilo, na ukawataka wananchi wavute subira, si watavuta subira tu, kwani watafanya nini? Baada ya nusu mwaka, mwaka mmoja, au miaka mitatu ijayo utawaambia nini tena?

Katika kampeni hii iliyoanza Jumamosi iliyopita ni dhahiri tutajifunza mengi. Kwa mfano sasa najua kwamba iko mipango ya kuanzisha usafiri wa reli jijini Dar es Salaam. Utaanza lini, na utahusu maeneo gani tutakuja kujua baadaye. Lakini tunakumbuka kwamba zaidi ya miaka kumi iliyopita tuliambiwa kuhusu mabasi yaendayo kasi jijini Dar es Salaaam; leo ndiyo tunaona barabara zinajengwa kwa kusuasua. Hiyo reli ni ya mwaka ujao au ya miaka 15 ijayo? Na wala wazo hili la reli si jipya! 

Ingewasaidia wakuu wetu kama wangekuwa na utaratibu wa kuketi pamoja, katika vikao vya chama, na kujadili masuala yote makuu ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni kabla ya kutoka kwenda Jangwani kutoa ahadi nyingine.

Wapinzani hawana la kuthibitisha kwa sababu hawajakamata madaraka. Chama-tawala ndicho kilichobeba mzigo wa kuthibitisha kimefanya nini katika kipindi chote cha utawala wake kabla hakijasema kinadhamiria kufanya nini na kutoa ahadi nyingine zitakazokuja kuwa kitanzi kwake.

Ushauri wangu: Punguzeni ahadi; tekelezeni zile mlizokwisha kuahidi.
Chanzo: Raia Mwema

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits