CHAMA cha Wananchi (CUF), kimedai kushangazwa na kauli iliyotolewa na
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Bw. Nape Nnauye kwa vyombo vya
habari kuwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimeingia
mikataba ya kifisadi na wafadhili wa nje ili kupora rasilimali za nchi.
Taarifa iliyotolewa Dar es Salaama jana na Naibu
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CUF, Bw. Abdul Kambaya, alisema Bw.
Nnauye hakupaswa kuishtaki CHADEMA kwa wananchi bali kupitia Serikali
yao walipaswa kuzuia fedha hizo na kuwataja wafadhili hao.
“CUF
kimeshangazwa na kauli hii ambayo imetolewa na msemaji wa CCM, ambacho
ndio chama kinachoongoza nchi, tulitarajia Bw. Nnauye angewataja hao
wafadhili wa CHADEMA ambao dhamira yao ni kupora rasilimali za nchi,”
alisema Bw. Kambaya.
Aliongeza kuwa, chama hicho kinaamini CCM na
CHADEMA ni watoto wa familia moja ambapo wafadhili wao ndani na nje ya
nchi pia wa aina moja.
“Kama CHADEMA imeingia mikataba ya kupewa
mabilioni ili baadae wataposhika madaraka waweze kulipa mabilioni hayo
kupitia rasilimali za nchi basi watakuwa wanaendeleza utaratibu wa CCM
kuingia mikataba mibovu isiyo na tija kwa Watanzania,” alisema.
Alisema
CUF inaamini kuwa, tatizo lililopo nchini ni mifumo mibovu
inayoendesha Serikali, nchi, kukithiri kwa wizi, matumizi mabaya ya
fedha za umma na ukiukwaji wa haki za binaadamu.
Bw. Kambaya
alisema, sababu ya Watanzania wengi kuwa maskini wa kutupwa, ukosefu wa
huduma bora kwa jamii, kudumaa kwa maendeleo ya nchi na ukosefu wa ajira
ni matokeo ya muda mrefu yanayosababishwa na mfumo mbovu uliopo.
Alisema
njia sahihi ya kulinda rasilimali zilizopo na zinazoendelea kugunduliwa
nchini Serikali ya Umoja wa Kitafa ambayo itashirikisha vyama vyote
vyenye wabunge.
Aliongeza kuwa, kwa kuzingatia utaratibu huo
hakuna chama ambacho kitakuwa na maamuzi yake katika matumizi ya
rasilimali na Maliasili za nchi.
“Sisi tunataka Watanzania
waelewe kuwa, mazingira yanaonesha CHADEMA kimeizidi kete chama tawala
kwa kuwa na wafadhili wa nje ndio maana CCM Inapiga kelele,” alisema.
Chanzo: Majira
Thursday, August 16, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment