Wednesday, August 22, 2012

Mwili wa Zenawi umewasili Adis Ababa

Best Blogger Tips
 Mwili wa aliyekuwa Waziri Mkuu wa Ethiopia, Melez Zenawi, uliwasili jana usiku katika mji mkuu wa nchi hiyo Adis Ababa na kwa sasa umehifadhiwa katika Ikulu hadi mazishi yake yatakapofanyika.

Maelfu ya raia wa nchi hiyo walimiminika katika barabara za mji huo jana jioni wakati mwili wake ulipowasili kutoka mji mkuu wa Ubelgiji, Brussels.

Meles, ambaye alikuwa na umri wa miaka 57, aliaga dunia ghafla kutokana na maambukizi wakati alipokuwa akitibiwa.

Kifo cha Bwana Zenawi kimezua hofu ya kugombea madaraka hali ambayo ingeweza kuathiri amani ya nchi hiyo.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari, naibu waziri mkuu Hailemariam Desalegn ataliongoza taifa hilo hadi mwaka 2015 wakati uchaguzi mkuu utakapofanyika.

Utawala wa Bwana Zenawi ulishutumiwa kwa kukandamiza upinzani na kuna hofu kuwa Waziri Mkuu mpya huenda asiwe na uzoevu wa kushughulikia na kutatua uhasama wa kisiasa unaoendelea nchini humo.

Zenawi amesifika kwa kuiongoza Ethiopia kufikia mafanikio makubwa ya maendeleo na uchumi, lakini wakosoaji wake wanasema licha ya hayo yote utawala wake haukuruhusu uhuru wa siasa za vyama vingi na kuwa viwango vya ukiukwaji wa haki za binadam bado viko juu.

Bwana Zenawi alikuwa kiongozi wa Ethiopia wakati taifa hilo lilipoingia vitani na nchi jirani ya Eritrea mwaka 1998.

Meles Zenawi aliingia madarakani mwaka 1991 baada ya mapinduzi lakini akapokea sifa kutoka kwa mataifa ya magharibi.
Chanzo: BBC

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits