Friday, August 10, 2012

Maelfu wamzika Atta Mills

Best Blogger Tips
 Maelfu ya wananchi wa Ghana jijini Accra wamehudhuria mazishi ya kitaifa ya rais John Atta Mills aliyefariki ghafla mwezi Julai mwaka huu.

Baadhi ya wakuu wa nchi za Afrika wapatao kumi na wanane na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Marekani Hillary Clinton walihudhuria mazishi hayo katika uwanja wa historia ya uhuru mjini Accra.

Mills aliyeugua saratani ya koo kwa muda mrefu amefariki ikiwa imebaki miezi mitano tu kabla ya kufanyika uchaguzi wa urais ambao angegombea tena nafasi hiyo.

Mwandishi wa BBC mjini Accra anasema kifo chake kimewaunganisha Waghana katika majonzi.
Anasema kifo hicho kilionekana kama jaribio kwa demokrasia changa ya nchi hiyo.

Mills aliyeanza kipindi cha miaka minne ya urais mwezi Januari mwaka 2009, amerithiwa na makamu wake rais John Dramani Mahama.

Ghana imepongezwa na jumuiya ya kimataifa kwa namna ambavyo imeshughulikia kipindi cha mpito katika taifa hilo linalofahamika kwa siasa zake za mgawanyiko.

Mazishi

''Leo giza nene limetanda katika anga ya Ghana, Afrika na kwa kweli ulimwengu mzima,'' Bwana Mahama aliuambia umati wa waombolezaji waliokuwa wakifuatilia mazishi hayo kupitia televisheni kubwa zilizowekwa uwanjani hapo.

''Rais Mills alikuwa muhimu sana katika yale ambayo tumekuwa hatuna katika siasa zetu, uzalendo, uvumilivu katika uongozi, uaminifu,'' alisema.

Mwandishi wa BBC Vera Kwakofi anasema watu walianza kukusanyika mapema alfajiri katika uwanja huo wakiwa wamevalia mavazi maalum ya maombolezo rangi nyeusi na nyekundu.

Machifu wengi wa kimila walihudhuria wakiwa na ngoma zao wakipiga midundo ya ujumbe wa kuomboleza.

Mbele ya wapiga ngoma wachezaji walichezesha mikono yao kwa namna ya ishara yenye maana maalum.

Wakati bendi ya jeshi ilipoingia na mwili wa marehemu uwanjani, ngoma, nyimbo za kusifu na za kishujaa zilisimama, mwandishi wetu anasema.

Filimbi za kuomboleza zilichezwa wakati rais Mahama alipowasha moto wa ishara ya kumbukumbu kwa marehemu, ambaye daima alitambulika kama ''Profesa au Mwalimu'', ikiashiria taaluma yake ya muda mrefu ya ualimu, na ''Asumdwoehene'', ikimaanisha mfalme wa amani katika lugha ya Twi.

Misururu ya foleni

Kwa muda wa siku mbili kabla maelfu ya wananchi wa Ghana walisafiri kuelekea Accra kutoa heshima zao za mwisho kwa mwili wa Mills.

Baadhi walipanga foleni kwa saa kadhaa, wengi wao wakilia kwa uchungu, katika mistari ya urefu wa kama kilometa kumi nje ya jengo la Ikulu mjini Accra.

''Nimekuwa hapa kwa saa tatu, ili kumuona, lakini tutamkumbuka sana hapa,'' mwanamke mmoja aliiambia BBC.

Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Marekani Hillary Clinton aliwasili Ghana akitokea Nigeria siku ya Alhamisi kuhudhuria mazishi hayo, akikamilisha ziara yake ya siku kumi na moja ya nchi saba za Afrika.

 Amefanya mazungumzo na rais Mahama. Ikionekana kama mfano bora wa demokrasia katika eneo hilo la Afrika, ghana ilichaguliwa na rais wa Marekani Barack Obama katika ziara yake ya nchi zilizo kusini mwa jangwa la sahara mwaka 2009.

Mills aliyefariki akiwa na umri wa miaka 68 alikuwa ni mwanasiasa wa ngazi ya juu kwa miaka mingi.

Kati ya mwaka 1997-2001 alikuwa makamu wa rais kwa aliyekuwa mtawala wa kijeshi Jerry Rawlings, lakini alijiweka mbali na kiongozi huyo.

Aliingia madarakani baada ya ushindi mwembamba dhidi ya mgombea kutoka kilichokuwa chama tawala cha New Patriotic Party, Nana Akufo-Addo
katika uchaguzi wa mwaka 2008.
Chanzo: BBC

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits