Friday, August 10, 2012

Ntagazwa afichua kilichomtoa CCM

Best Blogger Tips
 WAZIRI wa zamani wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira na Muungano), Arcado Ntagazwa, ameelezea sababu ya kuondoka Chama Cha Mapinduzi (CCM), akisema ni hofu ya kukosa jibu mbele ya Mwenyezi Mungu juu ya chama hicho kilivyoshindwa kuwatumikia Watanzania licha ya kuongoza nchi yenye utitiri wa rasilimali.

Ntagazwa aliyasema hayo jana wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika Kata ya Mbingu eneo la Tandale katika Wilaya ya Kilombero, mkoani Morogoro.

Alisema, katika mila na desturi za Kiafrika, kiapo kina thamani kubwa na anayeshindwa kukitimiza kiapo chake, basi laana huwa juu yake.

“Mimi nilikuwa CCM, nikiwa mbunge kwa miaka 25 na kushika nafasi mbalimbali za uongozi, ikiwemo ya naibu waziri na uwaziri kamili…Ndani ya ilani ya CCM, kuna ahadi, ahadi ya nne inasema sitopokea wala kutoa rushwa, hii ikiwa ni ahadi ya kila mwana CCM ambayo inakiukwa kwa kiwango kikubwa,” alisema Ntagazwa.

Aliongeza kuwa, shida zote zinazoipata Tanzania kwa sasa, ikiwemo hali ngumu ya maisha, walimu kukosa maslahi bora na ukosefu wa huduma muhimu za kijamii, ni matokeo ya kiapo hicho kukiukwa na viongozi wa CCM.

Alisema, kwa sasa ndani ya CCM hakuna wa kumuonya mwenzake juu ya kuachana na mfumo wa kutoa na kupokea rushwa, hivyo kutokuwa mwokozi kwa tabaka la wanyonge.

Ntagazwa alisema, kutokana na hali hiyo kuwa sugu ndani ya CCM, yeye kama mtu anayehofu ghadhabu za Mwenyezi Mungu, aliamua kujiengua na kuchagua kupigania Watanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

”Nilijua kuwa ipo siku Mwenyezi Mungu ataniita Ntagazwa… Ntagazwa nami nitamuitikia naam, swali litakalofuata ni je, ulitumiaje nafasi yako ya uongozi kwa Watanzania katika kuwatendea haki, ” alisema Ntagazwa huku wananchi wakimshangilia.

Alisema, kwa sababu ya ufisadi unaofanywa na Serikali ya CCM, leo hii kuna hatari kubwa ya vijana kuwa walemavu wa migongo (kibiongo) kutokana na kukaa chini muda mrefu wakiwa darasani  huku wakilazimika kutumia magoti yao kama meza ya kuandikia.
Chanzo: Tanzania Daima

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits