Tuesday, August 7, 2012

Shivji, Lwaitama wataka Muungano uvunjwe

Best Blogger Tips
 WASOMI na wanazuoni nchini wametaka Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, uvunjwe kwa kuwa waasisi wake walikuwa na maslahi yao binafsi.

Wakitoa mada kwa nyakati tofauti Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Azaveli Lwaitama, Prof. Abdul Sheriff wa Zanzibar na Prof. Issa Shivji waliushambulia Muungano huo.

Akitoa mada juu ya nguvu ya vyombo vya habari katika kutatua kero za Muungano, Prof Issa Shivji alisema, viongozi wanapindishapindisha historia ya Muungano na kuitumia kama kichaka cha maovu yao.

Aliongeza kuwa, hakuna Msahafu wa Muungano hivyo ulipaswa kuwa na mgawanyo wa madaraka kwa pande zote mbili, hivyo aliitaka tume ya Katiba kutoa fursa kwa wananchi ili watoe maoni yao juu ya suala la Muungano.

Pia alishauri kuwepo na demokrasia ya wazi na ukweli kwa ajili ya Watanzania juu ya suala hilo la Muungano.

Kwa upande wake, Dk. Lwaitama alieleza kuwa sio jambo la hekimu kuyalazimisha makundi ya watu kwa kutumia bunduki.

“Huu Muungano hata waliouanzisha hawakujua namna ya kufanya pale inapotokeza changamoto kama hizi za leo,” alisema na kuongeza kuwa, hakuna haja ya kung’ang’ania Muungano kwa kuwa lengo la waasisi lilikuwa ni kutengeneza taifa ambalo tayari limefanikiwa.

Awali, Prof. Sheriff alisema Zanzibar imepoteza imani na Muungano kutokana na muundo wake kuwa na matatizo tangu ulipoanzishwa.

Alitaka kutumiwa kwa fursa iliyopo ya marekebisho ya Katiba kwa lengo la kuungalia Muungano kwa jicho la tatu.

Alihadharisha vyombo vya habari kuacha kuandika habari za maovu na kuzipamba kama ilivyoripotiwa katika tukio la kikundi cha uamsho, ambapo wengi waliziandika bila kuwa na ufahamu wa kina.
Source: Mwananchi

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits