Sunday, August 5, 2012

Makamba: Maisha bora hayawezi kuletwa na JK

Best Blogger Tips
 BAADA  ya kimya cha muda mrefu, Katibu Mkuu Mstaafu wa CCM, Yusuf Makamba  ameibuka na kusema kuwa maisha bora kwa kila Mtanzania hayawezi kuletwa na Rais Jakaya Kikwete.

Amesema kuwa mbunge mzuri anaweza kutoka chama chochote iwapo Watanzania watashirikiana naye katika kuleta maendeleo ya eneo husika.

Makamba ametoa kauli hiyo ikiwa imepita muda mrefu tangu aibuke katika kikao cha Halmashauri Kuu ya chama hicho (Nec) na kumtuhumu Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye kwamba amekigeuza chama kuwa mali yake binafsi.

Katika kikao hicho Makamba alisema hatua ya Nape kugeuza chama hicho kama taasisi yake binafsi ndiyo ambayo imesababisha kikose mwelekeo.


Lakini jana wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam muda mfupi baada ya mwanaye, January ambaye ni Mbunge wa Bumbuli na Naibu Waziri wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia kufungua mkutano wa wakazi wa jimbo hilo, Makamba alisema maendeleo ya Watanzania yataletwa na wao wenyewe, kwa kufanya kazi.

Huku akizungumza baadhi ya maneno kwa lugha ya kisambaa na kunukuu baadhi ya vifungu vya biblia takatifu, Makamba alisema Watanzania wamekuwa wavivu wa kufanya kazi na kwamba kila kitu wanategemea kitafanywa na Rais Kikwete.

Makamba alisema kuwa kwa sasa kumezuka tabia ya baadhi ya Watanzania kuwatupia lawama viongozi kwa kushindwa kuwapa maisha bora.

Makamba, alisema kuwa maendeleo hayawezi kuletwa na mbunge peke yake bali kinachohitajika ni ushirikiano wa pamoja ili kuweza kutimiza lengo na ahadi mbalimbali alizotoa.

Alisema kuwa anashangazwa na baadhi ya Watanzania kuamua kumtupia lawama Rais Kikwete kuwa kashindwa kuleta maisha bora wakati hawana umoja wa kuunganisha nguvu katika kutatua changamoto zinazoikabili nchi.

“Hata kama CCM itaondoka madarakani na kuingia Chadema  bado Watanzania wataendelea kulia umaskini kwa kuwa hatuna tabia ya kushirikiana na kufanya kazi,” alisema Makamba.

Makamba alimwagia sifa mwanaye, January ambaye alikuwa akizindua Shirika la Maendeleo Bumbuli (SMB)ambalo alilianzisha baada ya kuwa mbunge mwaka 2010, kusema kuwa kijana huyo ni mfano wa kuigwa na Watanzania kwa kuwa katika kipindi kifupi cha uongozi wake jimboni humo ameweza kutekeleza ahadi mbalimbali.

Alisema kuwa wananchi wa Bumbuli hawakufanya makosa kumchagua mbunge huyo na kuongeza kwamba wanatakiwa kumpa ushirikiano ili kulifanya jimbo hilo kupiga hatua kimaendeleo.

Kwa upande wake, January wakati akiwakaribisha wakazi wa Bumbuli pamoja na waliotoka mikoa jirani, alisema kuwa wamekutana ili kuangalia namna ya kukabiliana na changamoto zilizopo jimboni humo.

Alisema kuwa siku zote maendeleo huletwa na wakazi waliopo mbali na nyumbani hivyo aliwaomba kuhakikisha kuwa na umoja ili kuondoa matatizo yaliyopo jimboni humo ikiwa ni pamoja elimu, afya, miundombinu na maji.

Alisema kwa upande wake atahakikisha BDC, linawasaidia wakazi hao katika masuala ya ajira na elimu.

Alisisitiza kuwa ili kuinua kiwango cha ufaulu katika jimbo hilo wamebuni njia ya kupandisha ufaulu wa wanafunzi kwani kuanzia sasa wameanzisha kambi ya wanafunzi zaidi ya 150 waliofanya vizuri katika mitihani yao ya mokono ili kuwanoa zaidi, lengo likiwa ni kuhakikisha wanafanya vizru katika mtihani wao wa mwisho.


Januari ambaye ni Naibu Waziri wa Sayansi na Mawasiliano, alisema kuwa wamegundua kuwa baadhi ya wazazi jimboni humo wamekuwa kikwazo cha wanafunzi kushindwa kufanya vema mitihani yao.

aliongeza kuwa  BDC imepata fedha kiasi cha Sh 730 milioni kwa ajili ya kukusanya na kununua mazao ya mboga mboga yaliyopo jimboni humo,  hatua ambayo itasaidia kununuliwa kipato cha wakulima.

Alisema hatua hiyo itakwenda sambamba na kukifufua kiwanda cha matunda cha Maweni ambapo mkulima ataweza kuuza mazao yao huko na kuepukana na madalali na kwamba vijana zaidi ya 120 watapata ajira.
Chanzo: Mwananchi

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits