Thursday, October 20, 2011

Muammar Gaddafi auawa

Best Blogger Tips
Muammar Gaddafi
KIONGOZI wa Libya, Kanali Muammar Gaddafi  ameuawa. Habari zilizotangazwa na waasi wa majeshi ya serikali walitoa taarifa hiyo muda mfupi baada ya kutangaza kuushikilia mji wa Sirte, alikozaliwa Gaddafi.

Wapiganaji wa waasi walifanikiwa kupiga picha kwa kutumia simu na kusambaza kwa baadhi ya vyombo vya habari. Walidai kuwa  alionekana katika karavati akitambaa  kujaribu kujificha katika kati mwa mji wa Sirte. Hata hivyo walimpiga risasi mguuni.

Mpiganaji wa waasi, Mohammed al Bibi aliwaambia waandishi wa habari kuwa  baada ya kumwona Gaddafi alisikika akiwaambia askari hao: "Usipige risasi, usipige risasi," huku akiwa katika harakati za kujisalimisha. Kumekuwa na habari za utata kwamba  alifariki dunia baada ya maumivu makali ya majeraha miguuni, huku wengine wakisema  bado yu hai.

Waasi hao walidai kuwa alikutwa akiwa na bastola ya dhahabu  huku akiwa amevalia sare ya jeshi rangi ya  khaki. Ofisa mmoja wa  Baraza la Mpito la Taifa,  Abdel Majid  Mlegta alisema Gaddafi alipigwa pia kichwani.

Alisema alipigwa risasi alipokuwa akijaribu kukimbia  huku mpiganaji mwingine akidai kuwa alipigwa risasi tumboni. Gaddafi na familia yake walikuwa mafichoni tangu  Umoja wa Majeshi ya  Kujihami ya nchi za Magharibi, (NATO), na majeshi ya waasi  kuanza kuishambulia Tripoli  katika kati ya Agosti mwaka huu. Tukio hilo limetokea siku moja baada ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Hillary Clinton  kufanya ziara nchini Libya na kusema kuwa ana imani Gaddafi atakamatwa au kuuawa.

WAASI WAMALIZA KAZI SIRTE

MAJESHI ya waasi  Libya yametangaza kumaliza kazi baada ya kufanikiwa kuuteka mji wote wa Sirte, nyumbani alikozaliwa kiongozi wa zamani wa nchi hiyo, Kanali Mummar Gaddafi. Askari hao walisema walifanya mashambulio ya nguvu yaliyodumu kwa muda wa dakika 90 jana asubuhi.

Hata hivyo baadhi ya askari wanaomtii Gaddafi bado wapo katika mji wa Bani Walid, kusini mashariki mwa Tripoli. "Hii ni siku ya mwisho ya mapigano," alisema Luteni Kanali Hussein Abdel Salam wa kikosi cha Misrata. Alisema  katika awamu ya mwisho ya mapambano, waliweza kuwaona askari wa Gaddafi wakiwa wamejificha ndani ya nyumba kadhaa wakiwa na bunduki na silaha nyingine za kivita.

Serikali mpya ya Baraza la Mpito lilisema kuwa litatangaza Libya kuanguka baada ya kuuchukua mji wa Sirte. Wakati huo huo, Uingereza imeitaka Algeria kutoa ushirikiano dhidi ya Libya kuhusu familia ya Gaddafi ambayo imeomba hifadhi nchini humo. Waziri wa Mambo ya Nje wa  Uingereza, William Hague alikuwa akizungumza na waandishi wa habari baada ya kufanya ziara nchini humo.

Mtoto wa kike wa Gaddafi, Aisha, kaka yake Hannibal na mama yao  Safiya  wamehifadhiwa  nchini Algeria. Katika mkutano huo wa pamoja  na Waziri wa Mambo ya Nje wa Algeria Mourad Medelci,  Hague alisema  Agleria haipaswi kusita iwapo hata mahakama ya uhalifu wa Kimataifa ukiomba lolote ni lazima isikilizwe.

Alisema ni vema Agleria ikafanya kazi kwa karibu na serikali ya mpito ili kuepuka migogoro inayoweza kujitokeza baadaye.

Hata hivyo kwa upande wake, Medelci alisema watu hao wamepewa hifadhi kwa sababu za kibinadamu  na hata serikali ya mpito ya Libya inatambua hilo.

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits