Tuesday, July 31, 2012

Mtikisiko

Best Blogger Tips
 NCHI imetikiswa. Mgomo wa walimu ulioanza jana katika sehemu mbalimbali nchini, umeathiri kwa kiasi kikubwa sekta ya elimu huku kukiwa na taarifa za matukio yasiyokuwa ya kawaida yaliyoambatana na mgomo huo usio na ukomo.

Katika sehemu mbalimbali nchini, walimu waliripotiwa kugoma kwa kutoingia madarasani na wengine walifika kazini na kusaini vitabu vya mahudhurio kisha kuondoka hali iliyosababisha wanafunzi kurandaranda ovyo katika sehemu za miji iliyo karibu na shule hizo.

Mjini Dodoma ,wabunge jana walimbana Naibu Spika, Job Ndugai wakitaka shughuli za Bunge zisitishwe ili kujadili mgomo wa walimu ambao umeanza rasmi jana nchi nzima, na kuziacha shule nyingi zikiwa na walimu wakuu na wakuu wa shule pekee.

Hata hivyo, Ndugai alisema Bunge lisingeweza kujadili suala hilo kwani tayari Serikali ilikuwa imelifikisha mahakamani baada ya kushindwa kuafikiana na walimu katika ngazi ya usuluhishi.Wakati hayo yakiendelea, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa amesema Serikali itafuta mishahara kwa walimu walioitikia mwito Chama cha Walimu Tanzania (CWT) wa kushiriki mgomo ambao alisema siyo halali.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Dk Kawambwa pia aliwaonya walimu ambao alisema wamekuwa wakiwabughudhi wenzao ambao waliamua kwenda kazini.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo akiwa Mjini Morogoro aliwaagiza wakuu wa shule za msingi na sekondari mkoani humo kuandaa orodha ya majina ya walimu wasiofika kazini Julai 30 na waifikishe kwa maofisa elimu wa wilaya kabla ya saa 2:00 asubuhi ya Julai 31.

Waandishi wetu katika sehemu mbalimbali nchini pia waliripoti kwamba katika baadhi ya shule, wanafunzi waliruhusiwa kurejea nyumbani mapema kwa maelezo kwamba hakukuwa na masomo.Hali hiyo ilizua kizaazaa kwani katika baadhi ya mikoa wanafunzi walicharuka na kuitisha maandamano hadi katika ofisi za maofisa elimu wa wilaya, wakitaka Serikali iingilie kati mgomo huo ili waendelee kusoma.

Kadhalika, baadhi ya viongozi na watendaji wa Serikali walinukuliwa wakitoa matamko ya kuwasihi au kuwaamuru walimu warejee madarasani, kauli ambazo hata hivyo, hazikubadili uamuzi wa walimu hao.

Wanafunzi waandamana
Maandamano ya wanafunzi yaliripotiwa katika Mji wa Tunduma, Mbeya ambako polisi walitumia mabomu ya machozi kuwadhibiti wanafunzi.

Wanafunzi wa shule mbalimbali za msingi katika Wilaya ya Mbozi mkoani humo waliandamana wakidai haki ya kufundishwa. Hata hivyo, maandamano hayo yaliingiliwa na vibaka ambao baadaye walivunja ofisi za Halmashauri ya Mji wa Tunduma na kuiba mali kadhaa kisha kuchoma nyaraka zilizokuwemo.
Tukio hilo lilitokea asubuhi wakati wanafunzi wa shule 14 za msingi zilizopo katika halmashauri ya Tunduma walipojikusanya na kufanya maandamano hadi nyumbani kwa diwani na baada ya kumkosa walielekea kituo cha polisi na baadaye ofisi katika hizo.

Katika manispaa ya Temeke, Dar es Salaam zaidi ya wanafunzi 400 wa shule nne za msingi wameandamana hadi katika Ofisi ya Ofisa Elimu wa Manispaa hiyo kupinga mgomo huo.
Wanafunzi wao ambao waliandamana walitoka  katika Shule za Msingi Bwawani, Mbagala Kuu, Mtoni Kijichi na Maendeleo.

Wilayani Tarime, Mara wanafunzi wa shule mbalimbali za msingi jana waliandamana hadi Ofisi ya Ofisa Elimu wa Wilaya hiyo na zile za CWT, wakidai haki yao za kupata elimu baada ya walimu kugoma kuingia madarasani na kisha kuwataka wanafunzi kurejea nyumbani.

Wanafunzi hao walisikika wakiimba na baadaye kuzungumza mbele ya Ofisa elimu wa Wilaya, Emmanuel Johnson kwamba kitendo cha walimu kugoma kufundisha kinawaathiri wao, hivyo waliitaka Serikali kuwalipa walimu madai yao ili waendelee na kuwafundisha.

“Watoto tunataka haki zetu, Watoto tunataka  kupata elimu,  watoto tunataka kusoma tunaomba walimu walipwe madai yao tuingie madarasani, watoto tusinyimwe haki yetu ya kupata elimu walimu wanapogoma waathirika ni sisi wanafunzi Serikali tatueni mgomo wa walimu,” walisema wanafunzi hao.
Johnson aliwatuliza wanafunzi hao na kuwaahidi kwamba atatatua tatizo hilo, hivyo kuwataka kurejea shuleni leo kuendelea na masomo.

Mkoani Pwani mgomo wa walimu ulisababisha maandamano yaliyowahusisha wanafunzi wa shule za msingi kadhaa katika Wilaya za Kisarawe, Mkuranga, Bagamoyo na Kibaha waliokuwa wakiishinikiza Serikali kusikiliza madai ya walimu ili wao waweze kupata haki yao ya kufundishwa.

CWT wanena
Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiel Olouch alisema mgomo wa walimu umefanikiwa kwa asilimia 90 nchi nzima na kwamba walimu katika mikoa mbalimbali hawakwenda kazini ikiwa ni hatua ya kushinikiza kupewa haki yao.

“Tunawashukuru walimu kwa kuunga mkono azimio lao ambalo walilipigia kura la kufanyika kwa mgomo na kubaki nyumbani bila ya kwenda kazi hadi pale Serikali itakaposikiliza matatizo yao” alisema Oluoch na kuongeza:

“Mgomo huu ambao umeanza leo (jana) hautahusiana na Sensa ya Watu na Makazi inayotarajiwa kufanyika usiku wa kuamkia Agosti 26, mwaka huu.”
Oluoch alisema kikomo cha mgomo huo ni pale itakapotolewa taarifa na Rais wa CWT, Gratian Mukoba na si mtu mwingine yeyote wala Serikali.

“Walimu wanatakiwa kutambua kuwa mgomo huu utaendelea hadi pale Rais Mukoba atakapowatangazia kinachoendelea hivyo kwa hivi sasa waendelee na mgomo huu,” alisema Oluoch.

Serikali yang’aka
Akizungumzia mgomo huo Dk Kawambwa alisema: “Tutatumia sheria kwa kushikilia malipo ya mishahara kwa walimu wanaogoma na tutatumia pia sheria kuwaadhibu walimu wanaowabughudhi wenzao kwa kuwalazimisha wagome.”

Alisema kwa mujibu wa Sheria ya Kazi ya mwaka 2004 ambayo vyama vya wafanyakazi vinaitumia kufanikisha migomo, Kifungu cha 83(4) kinaeleza kwamba mfanyakazi hatapaswa kulipwa mshahara katika kipindi chote ambacho itatokea amegomea utoaji huduma kwa umma.

Akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari, Dk Kawambwa alisema Kuwa Serikali itahakikisha kwamba inawalinda walimu wote ambao hawaungi mkono mgomo huo aliodai ni haramu kwa kuwa suala hilo kwa sasa linashughulikiwa mahakamani.

Katika hatua nyingine, Dk Kawambwa aliwaonya wazazi kuhakikisha kwamba watoto wao hawatumiwi na wagomaji kwa kuhimizwa kufanya maandamano  na vurugu.
Chanzo: Mwananchi

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits