Monday, July 25, 2011

Kikwete apunguza maofisa anaosafiri nao nje

Best Blogger Tips
RAIS Jakaya Kikwete ameridhia idadi ya maofisa katika ziara zake za nje ipunguzwe ikiwa ni hatua ya kupunguza gharama.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe aliliambia Bunge mwishoni mwa wiki wakati akijibu hoja ya kambi ya upinzani iliyoendelea kutaka safari za nje kwa viongozi zipunguzwe.

Membe alisema katika safari ya hivi karibuni ya Rais Kikwete nchini Shelisheli, idadi ya maofisa alioongozana nao ilikuwa 34 na kwa safari ya Afrika Kusini ilikuwa 34.

Hata hivyo, Waziri Membe alisema wakati mwingine, wingi wa maofisa huzingatia na aina ya ziara na nchi anakokwenda.

Alitoa mfano kwamba, endapo anakwenda nchi ambayo ulinzi wake upo shakani, idadi inaweza kuongezeka.

Alisema, zipo ziara nyingine kama vile za kibiashara inawezekana akalazimika kuongozana na ujumbe wa wafanyabiashara.

Awali, katika kuchangia hotuba ya makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yaliyopitishwa, kambi hiyo ya Upinzani kupitia kwa Waziri Kivuli wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Ezekia Wenje ilisema safari za viongozi wa juu zinatakiwa ziendane na hali ya uchumi.

Wenje alisema katika dhana ya kupunguza matumizi, baadhi ya safari za nje ambazo siyo lazima mkuu wa nchi kwenda, awaachie viongozi wengine washiriki kwa kuwa msafara wa Rais nje ya nchi una gharama kubwa ikilinganishwa na mawaziri au maofisa wengine wa Serikali.

“Kambi ya Upinzani inaitaka wizara ikishirikiana na ofisi ya Rais kuweka utaratibu wa safari za viongozi nje ya nchi, ili kupunguza matumizi makubwa ya Serikali na hatimaye fedha hizo zielekezwe katika miradi mbalimbali ya maendeleo,” alisema Wenje.

Hata hivyo, Serikali imekuwa ikisisitiza kwamba safari za Rais Kikwete nje ya nchi ni zenye manufaa na imekuwa ikitoa mafanikio ya ziara hizo katika nchi mbalimbali duniani.

Kwa mfano, Marekani ambako Rais Kikwete amekuwa na ziara tangu wakati wa utawala wa Rais George W. Bush na sasa Rais Barack Obama, Tanzania imenufaika kwa kupatiwa fedha nyingi katika miradi ya barabara, umeme, afya na maji.
Chanzo: HabariLeo

No comments:


Copyright 2011 Mambo ya Leo Blog. All Rights Reserved.
 

yasmin lawsuits